Radio Fadhila

MANAWASA yafanikiwa kufunga mita 95 za malipo ya kabla

19 March 2025, 10:55 AM

Mkurugenzi wa Huduma kwa wateja wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Masasi Nachingwea (MANAWASA) Obadia Mtuya. Picha na Godbless Lucius

“Wateja wa huduma ya maji wanazidi kuongezeka, na sisi kama taasisi tutaendelea kuboresha mifumo yetu ili kuhakikisha wateja wanapata huduma bora, na kuziba kabisa mianya ya ubadhirifu na kumfanya mteja awe salama anapotumia huduma za maji”

Na Neema Nandonde

Katika kuboresha upatikanaji wa huduma  ya maji safi na usafi wa mazingira, kuondoa malalamiko ya wateja kuhusu  kubambikiziwa ankara  za maji na changamoto ya wateja kulimbikiza ankara za maji, Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Masasi Nachingwea (MANAWASA),  imefanikiwa  kufunga mita za maji 95  za  malipo ya kabla  kwa baadhi ya  wateja zikiwemo taasisi.

Akizungumza Machi 18, 2025 kupitia kipindi cha Morning Booster kinachorushwa na redio Fadhila, kuelekea kilele cha maadhimisho ya wiki ya maji, Mkurugenzi wa Huduma kwa wateja MANAWASA Obadia Mtuya amesema  kuwa, wameanza kufunga mita hizo ikiwa ni utekelezaji wa agizo la rais Dkt Samia Suluhu Hassan ambalo pia litasaidia kuboresha upatikanaji wa huduma kwa wananchi.

Aidha ameongeza kuwa maeneo mengine yaliyoboreshwa ni pamoja na kituo cha kisasa cha miito ya simu kwa wateja cha bure na mifumo ya usomaji na ulipaji wa ankara za maji.

Sauti ya Mkurugenzi wa Huduma kwa wateja MANAWASA Obadia Mtuya

Sambamba na  hayo, Mtuya amewasihi wananchi wilayani Masasi kushirikiana  na MANAWASA katika kulinda vyanzo vya maji na kufichua  wahujumu wa miundombinu ya maji huku akiwasisitiza kulipa  ankara za maji kwa wakati, ili mamlaka hiyo iweze kujiendesha na kupanua mtandao wa maji kwa wateja wengine.

Sauti ya Mkurugenzi wa Huduma kwa wateja MANAWASA Obadia Mtuya