Radio Fadhila

TCRA yasisitiza matumizi ya namba 3 muhimu kudhibiti utapeli

11 April 2025, 2:52 PM

Mhandisi wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Kanda ya Mashariki Khatibu Chande, alipokuwa akizungumza kupitia redio Fadhila. Picha na Godbless Lucius

Namba 15040 mwananchi ataitumia  kuripoti  namba  za  mtu anayejihusisha  na  utapeli wa kimtandao na  namba hizo bure bila malipo yoyote.

Na Neema Nandonde

Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), imewataka wananchi kuendelea  kutumia  namba  3 muhimu, ambazo zinatumika katika kuzungumza na watoa  huduma  kwa  wateja  wa mitandao ya  simu, kuripoti namba za matapeli  na kuangalia  usajili wa namba ambazo zimesajiliwa kupitia kitambulisho cha taifa (NIDA).

Akizungumza na redio Fadhila kwenye kipindi cha Asubuhi cha Morning Booster, April 10, 2025 kuhusu kampeni ya NI RAHISI SANA na SITAPELIKI Mhandisi wa TCRA Kanda ya Mashariki Khatibu Chande, amezitaja  namba  hizo kuwa  ni namba 100, ambayo inatumika na mitandao yote  ya  simu  kuwasiliana  na  wateja, hivyo wananchi wasidanganyike na namba  za matapeli wanaojitambulisha kutoka kwenye mitandao ya simu.

Namba  nyingine  ni namba *106#, ambayo inatumika  kuangalia  namba ambazo zimesajiliwa  kwa  kutumia  kitambulisho cha taifa (NIDA) cha mwananchi husika, hivyo atakapoona namba asizozifahamu zikiwa zimesajiliwa kupitia kitambulisho chake, akatoe taarifa mapema kwenye duka la mtandao wa simu husika.

Aidha namba  ya  tatu ni 15040 ambayo mwananchi atatumia  kuripoti  namba  za  mtu anayejihusisha  na  utapeli wa kimtandao,  huku akisisitiza kuwa, mwananchi atatumia  namba hizo bure bila malipo yoyote.

Sambamba  na  hayo, Mhandisi Khatibu amewasisitiza wananchi kuacha tabia  ya kufungua viunganishi (links) hovyo, kutumie WIFI za bure ambazo huwajui  wamiliki wake, kwani ni rahisi kwa wezi wa mtandaoni na wadukuzi  kupata  taarifa za mtumiaji wa mtandao.