Radio Fadhila

WAZIRI wa Nchi ofisi ya Waziri mkuu,Geofrey Mwambe ametimza ahadi yake kutoa msaada wa umaliziaji wa jengo la msikiti

18 December 2021, 4:11 AM

WAZIRI wa Nchi ofisi ya Waziri mkuu, Uwekezaji ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Masasi, Geofrey Mwambe ( aliyevaa kanzu ya njano ) ametimza ahadi yake ya maombi ya Baraza la waislamu Tanzania (BAKWATA) Wilaya Masasi lililomtaka kutoa msaada wa umaliziaji wa jengo la ujenzi wa msikiti mkuu wa wilaya ya Masasi ambao ulianza kujengwa mwaka 2017 na kushindwa kukamilika kwa kukosa fedha za umaliziaji wa ujenzi huo.

Kutokana na ufanikishaji huo alioufanya Waziri Mwambe kwa kumpata mfadhili huyo wa kukamilisha ujenzi wa msikiti huo waislamu wilayani Masasi wameamua duwa maalumu ya Kumshukuru waziri Mwambe pamoja na mfadhili huyo ambaye ni Bakharesa, dua hiyo imefanyika leo msikiti mkuu wa BAKWATA Masasi huku waziri Mwambe akiwa mgeni rasmi katika hafla hiyo ya duwa maalumu.

Fedha ambazo zilikuwa zinahitajika ili kukamilisha ujenzi huo ni zaidi ya Sh.milioni 500 ambapo kupitia maombi ya waislamu hao kwenda waziri Mwambe na waziri huyo kuyachukua na kuyafanyia kazi yalizaa matunda baada ya waziri Mwambe kufanikisha kumpata mfadhili atakaye beba ghalama zote za ujenzi wa kukamilisha ujenzi huo ambaye ni Saidi Salim Bakharesa kwa kukubali kutoa fedha hizo zote zaidi ya Sh.milioni 500

Aidha, waislamu hao pia kupitia dua hiyo waliyoifanya hii leo wamemshukuru Bakharesa kwa kukabali kusaidia ujenzi wa msikiti huo hadi kukamilika kwake.

Msikiti huo ambao ulikuwa ukijengwa kwa michango ya waislamu wenyewe na baadaye kushindwa kukamilika kutokana na kasi ya utoaji wa michango ya ujenzi kuwa ndogo ndipo waislamu hao walipomuita Waziri Mwambe mwaka huu siku ya baraza la Eddi na kumuomba msaada wa kifedha au kusaidia upatikanaji wa mfadhili atakaye ridhia kutoa msaada wa kukamilisha ujenzi wa msikiti huo wa wilaya.

Waziri Mwambe alitumia fursa hiyo kuwataka waislamu na wanamasasi kwa ujumla kuwa kitu kimoja katika kuijnega Masasi kiuchumi na kijamii na kwamba yeye akiwa kama Mbunge wao atahakikisha anaendelea kupambana ili kuleta maendeleo.

Aidha, waziri Mwambe pia ni Mbunge Jimbo la Masasi alielezea mafanikio yaliyopatikana Masasi hadi sasa na mikakati iliyopo, baadhi ya mafanikio hayo ni upatikanaji Barabara za lami ambazo zingine zinaendelea kujengwa, maji safi na salama, afya na elimu.