Radio Fadhila

MKUU wa Wilaya ya Masasi mkoani Mtwara, ameomba kupewa ushirikiano wa karibu kutoka kwa watendaji

9 July 2021, 7:25 AM

MKUU wa Wilaya ya Masasi mkoani Mtwara, Claudia Kitta( katikati) ameomba kupewa ushirikiano wa karibu kutoka kwa watendaji na wananchi wa wilaya hiyo ili kwa pamoja kuweza kufanya kazi kwa bidii katika kutatua kero za wananchi wa wilaya ya Masasi.

Mkuu huyo Mpya wa Wilaya ya Masasi amesema hayo 1 mara baada ya kukabidhiwa rasmi Ofisi na aliyekuwa mkuu wa Wilaya hiyo, mbaye kwa sasa ni mstaafu katika nafasi hiyo, Selemani Mzee , (aliyevaa barakoa) hafla hiyo ya makabidhiano ya ofisi na kumuaga mkuu wa Wilaya Mstaafu, Selemani Mzee, imefanyika katika viwanja vya ofisi ya mkuu wa wilaya Masasi maarufu kama Bomani.

Kitta amesema anahitaji ushirikiano baina yake na watendaji wote wa serikali na taasisi zisizo za serikali pamoja na wananchi kwani kufanya hivyo jitihada za kuleta maendeleo ndani ya Masasi zitaonekana.

Mkuu huyo Mpya wa Wilaya ya Masasi amesema kuwa anamshukuru Rais Samia Suluhu kwa kumteua kuwa mkuu wa Wilaya ya Masasi kwani tangu amekuja Wilaya ya Masasi amepokelewa vizuri na ni wazi kuwa watendaji na wananchi wa Masasi wameonyesha ukarimu wa hali ya juu katika kutaka kushirikiananae katika kuijenga Masasi.

Kwa upande wake,mkuu wa Wilaya mstaafu , Selemani amewapongeza wanamasasi kwa ushirikiano waliompa kipindi akiwa mkuu wao wa Wilaya hadi anastaafu na kuomba ushirikiano huo pia kumpa mkuu wa Wilaya aliyopo kwa sasa.