Loliondo FM

Kikao kamati ya lishe,wajane waondolewa kwenye nyumba yao Sale

1 August 2024, 3:44 pm

Mkuu wa wilaya ya Ngorongoro Kanali Wilson Sakulo akipitia taarifa ya lishe kwenye kikao cha kamati ya lishe.picha na Zacharia James.

Lishe ni kiasi na aina ya chakula unachokula kulingana na mahitaji ya mwili wako na lishe bora inamaanisha kuwa kiasi sahihi cha virutubishi vya mwili huliwa baadhi ya watu ula chakula kujaza matumbo na si kuzingatia lishe bora kwa mujibu wa wataalam wa afya.

Na Zacharia James.

Mkuu wa wilaya ya ngorongoro Mhe. Kanali Wilson Sakulo ameagiza utekelezaji wa viashiria vya lishe uendane na uhalisia wa hali ya lishe katika ngazi ya jamii.

Ameyasema hayo jumatano Julai 31, 2024 alipoongoza kikao cha kamati ya lishe ya wilaya ya Ngorongoro robo ya nne yani Aprili hadi Juni ambapo amewasihi watendaji wa kata kuhakikisha jamii inapata elimu juu ya lishe na umuhimu wake kwa maendeleo ya jamii kwani wao ndio wasimamizi na watekelezaji wa mkataba wa lishe ngazi ya jamij kwakua halmashauri ya wilaya ya Ngorongoro imeendelea kufanya vizuri ngazi ya mkoa kwa kutekeleza vyema na kwa ufanisi viashiria hivyo vya vya lishe .

Katika hatua nyingine Mhe.Sakulo amewasihi watendaji wa vijiji kuyajali na kuyasaidia makundi maalumu hasa wanawake wajane katika k kutatua changamoto zinazo wakabili ikiwemo kuwasaidia wapate ofisi ili kutekeleza shughuli zao katika kata ,kwani si kwa mapenzi yao kwamba wamefiwa na wenza wao huku akitolea mfano tukio la wajane katika kata ya Sale ambao wameondolewa katika nyumba ambayo walipewa na kata kuendesha shughuli zao licha ya kutumia zaidi ya shilingi milioni 1.3 kuikarabati ila wameondolewa bila kurudishiwa pesa yao wala kupewa mahala pengine pakufanyia shughuli zao za kujiinua kiuchumi na kujipatia kipato.

Sauti ya Kanali Wilson Sakulo

Kwa upande wake afisa lishe wa halmashauri ya wilaya ya Ngorongoro Salum Ally Juma amesema katika kipindi cha Aprili hadi Juni 2024 jumla ya watoto 35,503 wamepimwa hali ya lishe kwa kupimwa uwiano wa uzito kwa umri kupitia vituo vya kutolea huduma za Afya.

Amesema jumla ya watoto 33,004 sawa na asilimia 92.96 walikuwa na hali nzuri ya lishe, watoto 2,410 sawa na asilimia 6.79 waligundulika kuwa na hali hafifu ya lishe na watoto 89 sawa na asilimia 0.25 walikuwa na hali mbaya ya lishe .

Ametaja maeneo yenye watoto wenye hali mbaya ya lishe ni kata ya Olibalbal kati ya watoto 489 watoto 7 wana hali mbaya ya lishe, kata ya Nainokanoka kijiji cha Erkeepus kati ya watoto 1,283 watoto 19 wana hali mbaya ya lishe, na kata ya Malambo kati ya watoto 2,566 watoto 10 wana hali mbaya ya lishe, kata ya Ngorongoro kijiji cha Oloirobi kati ya watoto 376 watoto 6 wana hali mbaya ya lishe na kijiji cha Sero kata ya Ololosokwan kati ya watoto 454 watoto 7 wana hali mbaya ya lishe.

Sauti ya afisa lishe