Triple A FM

Mbinu za Fountain ‘kuiua’ Simba zawekwa wazi

18 September 2025, 5:34 pm

Mchezaji wa Mbeya City Omary Chibada (mwenye bandeji kichwani) akiwatoka wachezaji wa Fountain Gate Hassan Mey (Kulia) na Mudrik Shehe (Kushoto) Picha na Joel Headman

Na Joel Headman

Wazee wa Kikombe cha bati, chai ya moto leo wamekiona cha moto kutoka kwa Purple Nation Mbeya City kwenye mchezo wa 3 wa ligi kuu uliomalizika jioni hii hapa Tanzanite Kwaraa Babati

Kipute hicho kilianza majira ya saa 8 mchana kwa kasi kubwa, kikishuhudia Fountain Gate wakiipelekea moto kwelikweli Mbeya City bila mafanikio mpaka kipindi cha kwanza kinamalizika wakiwa wamepiga mashuti 2 tu langoni kwa mkongwe Beno Kakolanya na mengine 5 yakienda nje

Kipindi cha pili kilianza vile vile kama cha kwanza lakini mashambulizi yakawa kwa zamu na kunako dakika ya 54 Mchezaji Shaaban Pandu alimfanyia madhambi Habib Kyombo wa Mbeya City ndani ya 18 na mwamuzi wa kati Abel Willium akaamuru pigo huru la penalty ambalo lilikwamishwa kimiani na Habib Kyombo dakika 56

Mabadiliko matatu yaliyofanywa na Mbeya City yalionekana kuwaelemea Fountain Gate iliyokuwa na wachezaji wa 3 tu wa akiba (kipa akiwemo) na kuwafanya wapinzani wao kuutawala mchezo mpaka ukamalizika kwa goli 1 kwa sifuri

Kocha wa Fountain Gate Denis Kitambi amesifu bidii za wachezaji wake na kukiri kuwa bado wana kazi ya kufanya kurekembisha makosa yaliyojitokeza wakati wakisubiri utawala kushughulikia mambo yaliyokwamisha wachezaji wengine kucheza

Kwa upande wake Mwalimu wa Mbeya City Malale Hamsini akijivunia majina ya wachezaji wake na uzoefu wao kwenye ligi ameshukuru kwa kile kilichofanyika na kueleza kuwa bado wana kazi zaidi ya kufanya

Mwalimu wa Mbeya City Malale Hamsini

Timu zote 2 zitakuwa ugenini raundi ya 2 ya ligi kuu ambapo Mbeya City watakuwa wageni wa Azam na Fountain wakialikwa na Simba SC

Kocha wa Fountain amesema wataandaa mbinu kabambe za kumkabili mnyama na miongoni mwa hizo ni kumtazama kwa makini wikiendi hii akipepetuana na Gaborone United ya Botswana kwenye michuano ya CAF

Kocha wa Fountain Gate Denis Kitambi