Ruangwa FM

Wananchi kata ya Mbekenyera waridhia kutoa eneo ujenzi shule ya sekondari

7 July 2023, 4:51 pm

Wananchi kata ya Mbekenyera wilayani Ruangwa mkoani Lindi wameridhia kutoa maeneo zaidi ya hekari 30 pamoja na kushiriki katika nguvu kazi za ujenzi wa shule ya sekondari tarajiwa inayotajwa huenda ikaja kuitwa shule ya sekondari Nambawala.

Hatua hiyo inakuja kufuatia kata hiyo kupokea kiasi cha fedha shilingi milioni 560 za ujenzi wa shule mpya ya sekondari katani hapo kupitia mradi wa kuimarisha ubora wa elimu ya sekondari (SEQUIP).

Akiongea na wananchi wa kata ya Mbekenyera Julai 7 mwaka huu kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Ruangwa, Afisa elimu sekondari wilayani humo Mwalimu Ernest Haule ametoa shukrani kwa wananchi wa kata hiyo kwa kukubali kutoa eneo litakalojengwa shule hiyo na kuwaomba kuwa walinzi wa vifaa vya ujenzi wakati mradi huo utakapoanza kutekelezwa.

“Kila kila mmoja akawe mlinzi wa vifaa vya ujenzi ili kudhibiti wizi, vifaa vingi huwa vinaibiwa wakati ujenzi unaendelea tuache tabia hiyo” alisema Haule.

Kwa upande wake kaimu Mhandisi wa wilaya Philemon David amebainisha aina ya ujenzi hiyo inategemewa kuwa ya force account lakini itatumia mzabuni ambapo wananchi watakua miongoni mwa kamati mbili kamati ya mapokezi na kamati ya ujenzi huku akianisha kuwa watalaam wa Halmashauri watakua wafuatiliaji kupita kugagua maendeleo ya mradi katika kila hatua wakati ujenzi utakapokua unaendelea.

“Sisi kazi yetu kama halmashauri hasa wataalamu ni kupita na kushauri katika kila hatua ya ujenzi wakata mradi unaendelea” alisema Mhandisi Philemon

Baadhi ya wananchi wa kata hiyo akiwamo Omari Mohamed, na Hamisi chimale ambae ni Diwani wa kata hiyo wamesema wameupokea mradi huo na kwamba wako tayari kushiriki kuchangia nguvu kazi hatu ili kukamilisha kwa wakati mradi huo.

Kata ya mbekenyera inatajwa kuwa na jumla ya shule tisa za msingi na kusbabisha kuwa na idadi kubwa ya wanafunzi wanaofaulu Kwenda sekondari moja ambayo haitoshelezi hatua hiyo imepelekea kuwa na uhitaji mkubwa wa shule nyingine katani humo.