Adhana FM

Klabu ya michezo ya wazee Arusha, Baraza la wawakilishi wafurahishwa na kasi ya maendeleo Kaskazini Unguja

9 June 2024, 3:53 pm

Na Nishan Khamis.

Mkuu wa mkoa wa Kaskazini Unguja, Rashid Hadid Rashid amewapongeza umoja wa klabu ya michezo ya Wazee wa Arusha na klabu ya michezo ya baraza la wawakilishi kwa kutembelea ya mkoa huo.

Hadid ameyasema hayo leo huko ofisini kwake Mkokotoni wilaya ya Kaskazini “A” Unguja wakati akizungumza mara baada ya kuwasili ugeni huo kwa lengo la kutembelea miradi ya serikali na sehemu za kitalii katika mkoa huo.

Mhe, Hadid amesema katika kipindi cha miaka mitatu cha Daktari Husein Mwinyi ameimarisha sekta ya elimu ,vituo vya afya, barabara na miundombinu ya maji ikiwa ni mikakati ya serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya uongozi wa Dkt Samia Suluhu Hassan na serikali ya mapinduzi ya zanzibar katika kuimarisha upatikanaji wa huduma bora kwa wanachi.

Nae, katibu wa kilabu ya michezo ya baraza la Wawakilishi (BLSP) Nassor Salim Ali, amesema uhusiano huo umekuwepo zaidi ya miaka ishirini ambao umepelekea mafanikio baina ya watu wa mkoa Arusha na Zanzibar katika kukuza na kuendelea uhusiano wa kimaendeleo.

Kwa upande wake katibu wa kilabu ya michezo ya wazee wa Arusha, amempongeza mkuu wa mkoa kwa mapokezi mazuri pamoja na kufurahishwa na kasi ya maendeleo ya Zanzibar katika kipindi cha miaka mitatu kwa kuimarisha miundo mbinu ya afya, elimu, maji na barabara.