Kahama FM
Kahama FM
July 28, 2025, 6:06 pm

”Jamii inapaswa kujikita zaidi katika kujikinga dhidi ya maradhi ya ugonjwa wa homa ya ini kwa kuwa ni ugonjwa hatari na unaochukua maisha ya watu wengi duniani”
Na John Juma
Wananchi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kahama mkoani Shinyanga wamehimizwa kupima afya zao mara kwa mara ili kujikinga na maambukizi ya ugonjwa wa homa ya ini.
Hayo yamesemwa na mratibu wa shughuli za chanjo kutoka Manispaa ya Kahama Agnes Ndamaishinji, wakati akizungumza na Kahama FM, ikiwa leo ni Siku ya Maadhimisho ya Homa ya Ini Duniani.
Ndamaishinji amesema kuwa jamii inapaswa kujikita zaidi katika kujikinga dhidi ya maradhi ya homa ya ini kwa kuwa ni ugonjwa hatari na unaochukua maisha ya watu wengi duniani.
Aidha, Ndamaishinji amewataka wananchi kufika haraka katika vituo vya afya pindi wanapohisi kuwa na dalili za ugonjwa huo na kuwasisitiza juu ya namna bora ya kujikinga na ugonjwa wa homa ya ini kwa kila mtu.

Nao, baadhi ya wananchi wakizungumza katika nyakati tofauti tofauti, akiwemo Fatuma mayor, Jeremia Angelo na Juliana Edward wamesema kuwa wengi wao hawakuwa na uelewa wa kutosha kuhusu homa ya ini na kutoa wito kwa mamlaka husika za afya kuhakikisha elimu hiyo inawafikia wa jamii na kuokoa maisha ya watu.

Maadhimisho ya Homa ya Ini hufanyika Julai 28 kila mwaka, na kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) mtu mmoja hupoteza maisha kila baada ya sekunde 30, na watu 6000 hupata maambukizi mapya kila siku na kauli mbiu ya mwaka huu 2025 ‘‘ondoa vikwazo, tokomeza homa ya ini’’
