Tumbatu FM

Wafanyabiashara endeleeni kulipa kodi-ZRA

15 June 2024, 12:47 pm

Picha ya Meneja wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Kikodi  wa Mamlaka Ya Mapato Zanzibar (ZRA) Ndugu, Hanii Mohamed Khamis (asiyevaa kofia).

Nimuhim kwa wafanyabiashara kulipa kodi kwa maendeleo ya taifa.

Na Abdul Sakaza.

Mamlaka Ya Mapato Zanzibar (ZRA) imewataka wananchi na wafanyabiashara wa Mkoa wa Kaskazini Unguja kuendelea kulipa kodi ili kuongeza pato la taifa. 

Ameyasema hayo Meneja wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Kikodi  kutoka Mamlaka Ya Mapato Zanzibar (ZRA) Hanii Mohamed Khamis wakati  alipokua akizungumza na Wananchi na wafanyabiashara wa Mkoa huo kupitia kipindi maalum cha  Radio Jamii Tumbatu FM.

Meneja Hanii, amesema kuna umuhimu mkubwa wa kulipa kodi ikiwemo kuongeza pato la Taifa ambalo huchangia kwa kiasi kikubwa katika kujenga miundombinu mbali mbali ya kijamii ikiwemo Barabara, Vituo vya Afya, Shule pamoja na Masoko ambayo husaidia ukuaji wa maendeleo Nchini 

Katika hatua nyengine amewataka  Wanachi na wafanyabiashara kudai risiti za kielektroniki wanaponunua bidhaa mbali mbali na kuacha kupokea risiti za kienyeji zinazoandikwa kwa mikono  ambazo zimepigwa marufuku  na Serikali Ya  Mapinduzi Ya Zanzibar kutumiwa na Wafanyabiashara 

Kwa upande wake Afisa elimu kutoka Mamlaka Ya Mapato Zanzibar (ZRA) Ndugu, Abdulshakur Ramadhan Simai ameweka bayana kua kwasasa wameazisha programu(APP) maalumu inayopatikana Play Store inayojulikana “ZRA FUNGUKA” ili kurahisisha kupokea maoni kwa wananchi na wafanyabiashara hapa nchini 

Nao Wananchi na Wafanyabiashara wa Mkoa huo walioshiriki kipindi hicho kwa njia ya simu  Kupitia Radio Tumbatu FM wameishukuru Mamlaka Ya Mapato Zanzibar( ZRA ) kwa kuwapa elimu kuhusu umuhimu wa kulipa kodi na kudai risiti za kielektroniki kwani walikua hawana elimu hiyo na wameahidi kuifanyia kazi elimu hiyo walioipata.