

March 22, 2025, 7:06 pm
”Mkulima yeyote anayelima zao la tumbaku ataondokana na hasara ya majanga mbalimbali ya asili baada ya kupata mkopo wenye bima ya mazo kutoka benki ya NMB”
Na Sebastian Mnakaya
Wakulima wa zao la tumbaku wilayani Kahama mkoani Shinyanga wametakiwa kuchangamkia fursa ya kupata mikopo ya mazao yenye bima kutoka benki ya NMB ili kuondokana na hasara za majanga mbalimbali yanayotokea.
Haya yamesemwa leo na meneja mahusiano Kilimo kutoka benki ya NMB anayesimamia zao la tumbaku nchini Jacob Laurian katika mkutano mkuu wa 29 wa mwaka wa KACU, ambapo amesema kuwa kwa mkulima ambaye analima bila ya bima ya mazao yuko hatari kupoteza alichowekeza.
Aidha Laurian amesema kuwa mpaka sasa kupitia bima hiyo walitenga kiasai cha shilingi bilioni 1.2 kwa ajili ya kufidia zaidi ya wakulima 2000 kutokana na majanga mbalimbali yaliyokumbana nayo mwaka uliopita 2024.
Nae mwenyekiti wa Chama Cha Kikuu Cha Ushirika wilaya ya Kahama (KACU) Emmanuel Nyambi amesema kuwa wakulima wanapaswa kupewa elimu ya kutoa juu ya bima ya mazao ili wengi waanze kuitumia kwa ajili ya kuondokana na hasara za majanga ya asili yanayotokea katika maeneo yao.
Kwa upande wao baadhi ya wakulima wa zao la pamba na tumbaku kutoka vyama mbalimbali vya msingi akiwemo Zawadi Mashauri na Mwaja Doto kutoka halmashauri ya Ushetu na Msalala wameeleza namna wanavyonufaika na bima ya mazao inayotolewa na benki ya NMB ambayo imewasaidia kuondokana na changamoto ya kupata hasara ya majanga walioyapata.
Mpaka sasa benki ya Nmb imetoa mikopo kwa wakulima wa zao la tumbaku nchi nzima zaidi ya shilingi bilioni 270, huku mwaka jana wametoa fidia ya shilingi Billion 1.2 kama sehemu ya hasara kwa wakulima walipata majanga mbalimbali.