

February 28, 2025, 11:14 am
Serikali imesema itaendelea kushirikiana na sekta binafsi katika kuhakikisha Watanzania wanaendelea kupata huduma bora sambamba na kupunguza umasikini miongoni mwao
Na Sebastian Mnakaya
Serikali imesema itaendelea kushirikiana na sekta binafsi katika kuhakikisha Wantanzania wanaendelea kupata huduma bora sambamba na kupunguza umasikini miongoni mwao.
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri Mkuu ambaye pia ni Waziri wa Nishati Dkt. Doto Biteko katika hafla ya uzinduzi wa Benki ya Exim tawi la Kahama mkoani Shinyanga ambapo ameitaka Taasisi hiyo kufanya kazi bila matabaka ili kuwainua kiuchumi wafanyabiashara wenye mitaji midogo.
Dkt. Biteko ametaja manufaa kuwa ni kuongezeka kwa fursa za uchumi kwa kuongeza ajira, kuongeza mapato ya benki na hivyo kutumia sehemu ya faida yake kuchangia maendeleo ya jamii ikiwemo kusaidia makundi maalum kadhaa yenye uhitaji yaani (CSR)
Nae, Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Anamringi Macha amesema kuwa ufunguzi wa tawi la benki hiyo ni kielelezo kuwa shughuli za uchumi ni nyingi na zitaendelea kuimarishwa, huku, Mtendaji Mkuu wa Benki ya Exim Jaffari Matundu akisema kuwa uzinduzi wa tawi hilo unathibitisha dhamira yao ya kukuza ujumuishi wa kifedha na uwezeshaji wa kiuchumi kwa Wananchi na taifa kwa ujumla.
Naye, Kamishna wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha kutoka Wizara ya Fedha, Dkt. Charles Mwamwaja amesema kuwa Serikali imeendelea kuweka mazingira mazuri ya kifedha na kuwa dira iliyopo imekuwa ikiwaongoza na ni mpango mkuu wa sekta ya fedha ulioandaliwa na Serikali umeweka mazingira wezeshi na moja ya manufaa yake ni kufunguliwa kwa tawi hilo la benki.