Kahama FM
Kahama FM
March 6, 2026, 7:29 pm

Halmashauri ya Manispaa ya Kahama mkoani Shinyanga imetoa shilingi milioni 15 kwa kila kata kwa ajili ya ukarabati wa barabara, huku fedha hizo kwa kata ya nyahanga zikitengwa kwa ajili ya mitaro pembezoni mwa barabara.
Akizungumza na wananchi wa mtaa wa mtakuja wakati wa kikao cha kujadili maendeleo ya kata hiyo, diwani wa kata Nyahanga Josephine Kilimba amesema kuwa ili kuwa na barabara zenye ubora fedha hizo zitajenga mitaro katika barabara korofi ili ziwe imara katika kipindi hichi mvua nyingi zinazoendelea kunyesha.
Aidha, Kilimba amesema kuwa badala ya fedha hizo kukwangua barabara ni bora zikajenga mitaro, huku akisema kuwa watawatafuta wadau mbalimbali wa maendeleo kwa ajili ya kupata mifuko ya saruji na mawe ili kukamilisha ujenzi huo.

Nao, baadhi wa wananchi wa mtaa wa mtakuja wakizungumza kwa nyakati tofauti akiwemo Patrick Cosmas na Juma Salum, wamemshukuru diwani Kilimba kwa kufanya maamuzi hayo ya kujenga mitaro badala kukwangua ili kuondokana na changamoto ya mara kwa mara kwa ubovu wa barabara hizo.
Ikumbukwe, Halmashauri ya Manispaa ya Kahama kupitia baraza la madiwani wametenga shilingi milioni 300 kwa kata 20 za Manispaa hiyo kila mwaka, kwa ajili ukarabati wa barabara za mtaani na vijiji ili kupunguza changamoto ubovu wa barabara
