Kahama FM
Kahama FM
February 6, 2025, 10:46 pm

Mvua zinazoendelea kunyesha katika halmashauri ya Ushetu zimesababisha ukuta wa nyumba kupata unyevu na kusababisha kuanguka kutokana na nyumba hiyo kutokuwa imara.
Na Leokadia Andrew
Mwanafunzi wa kidato cha tatu katika shule ya Sekondari ya Chona Halmashauri ya Ushetu Wilayani Kahama mkoani Shinyanga Pendo William (16) amefariki dunia kwa kuangukiwa na ukuta wa nyumba aliyokuwa amepanga wakati mvua zikiendelea kunyesha huku wenzake watatu wakijeruhiwa sehemu mbalimbali za miili yao.
Kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa shinyanga Janeth Magomi amethibitisha kutokea tukio hilo ambalo limetokea usiku wa february 5 2025 ambapo chanzo cha tukio hilo ni mvua zinazoendelea kunyesha
Aidha kamanda Magomi ametoa wito kwa walimu na wazazi kuweka utaratibu wa kukagua nyumba ambazo wanafunzi wamepanga ili kujiridhisha juu ya ubora wake
Akizungumzia tukio hilo mkuu wa wilaya ya Kahama Mboni Mhita amemwaagiza mkurugenzi pamoja na wakuu wa idara kufanya ufuatiliaji wa wanafunzi ambao wanaishi katika nyumba za kupanga kujiridhisha iwapo ni salama