Vwawa FM Radio

Mitazamo hasi yawapora wenye ulemavu fursa za maendeleo

June 9, 2025, 1:39 pm

Baadhi ya watoa huduma za afya wakipatiwa mafunzo ya Lugha ya alama. Picha na Stephano Simbeye.

Mitazamo hiyo ni ya kutowathamini kwa maumbile yao

Na Stephano Simbeye

Mitazamo hasi dhidi ya watu wenye ulemavu imeendelea kuwa mojawapo ya sababu zinazochangia kutowajumuisha ipasavyo katika shughuli za maendeleo ya jamii, hali inayosababisha vipaji vyao walivyopewa na Mungu kubaki bila kuendelezwa.

Kauli hiyo imetolewa Juni 6 mwaka huu na mwalimu wa wanafunzi wenye mahitaji maalumu kutoka Shule ya Msingi Mwenge, Magreth Ndunduru, wakati wa mafunzo ya lugha ya alama yaliyotolewa kwa watoa huduma za afya.

Mafunzo hayo ya siku mbili yameandaliwa na shirika lisilo la kiserikali la ADP Mbozi kwa kushirikiana na shirika la DSW chini ya mradi wa SAfA, na kufanyika katika ukumbi wa Simple Palace, uliopo mjini Vwawa, wilayani Mbozi, mkoani Songwe.

Sauti ya Mwalimu wa wanafunzi wenye mahitaji maalumu kutoka Shule ya Msingi Mwenge Magreth Ndunduru.

Naye, Mwenyekiti wa Chama cha Walemavu Mkoa wa Songwe, Abel Mwakajila, amesema bado zipo changamoto nyingi zinazowakabili watu wenye ulemavu wanapotafuta huduma za kijamii, ikiwemo ukosefu wa miundombinu rafiki na ugumu wa kufikika kwa maeneo muhimu.

Sauti ya Mwenyekiti wa Chama cha Walemavu Mkoa wa Songwe Abel Mwakajila.

Mwakajila pia ametoa wito kwa taasisi zote za umma na binafsi kuhakikisha zinarekebisha au kujenga miundombinu rafiki kwa wenye ulemavu, ili waweze kupata huduma kwa usawa.

Sauti ya Mwenyekiti wa Chama cha Walemavu Mkoa wa Songwe Abel Mwakajila.