Savvy FM
Savvy FM
September 2, 2025, 4:48 pm

Mtendaji wa Kata ya Sakina, mkoani Arusha, anatuhumiwa kuhamisha baadhi ya fedha za miradi ya maendeleo na kuziweka kwenye akaunti yake binafsi, hali iliyosababisha kusimama kwa ujenzi wa kivuko muhimu kwa wakazi wa eneo hilo.
Na Jenipha Lazaro
Tuhuma hizo zimetolewa na baadhi ya viongozi wa mitaa husika, akiwemo mwenyekiti wa mtaa wa Mairiver Innocent Mboyo Loda mjumbe wa mtaa huo pamoja na mwenyekiti wa mtaa Melamari Joji Mollel, viongozi hao wamesema kuwa licha ya juhudi zao za kufuatilia matumizi ya fedha hizo, hawajawahi kupata maelezo ya kuridhisha kutoka kwa mtendaji huyo.
Wakizungumza mapema leo na Savvy FM, viongozi hao wamesema kuwa ujenzi wa kivuko hicho umeachwa katika hatua ya awali, jambo ambalo limekuwa kero kubwa kwa wananchi wa mitaa hiyo. Wamesema kuwa wakazi wa maeneo hayo, wakiwemo watoto, wajawazito na wazee, wamekuwa wakipata ajali mara kwa mara wanapojaribu kuvuka eneo hilo.
Kwa upande wao, wananchi wa mitaa hiyo wameiomba serikali kuingilia kati na kumalizia ujenzi wa daraja hilo, wakieleza kuwa hali ya sasa ni hatarishi kwa maisha yao, hasa kwa makundi maalum kama watoto, wanawake wajawazito na wazee ambao wamekuwa wakianguka mara kwa mara wakivuka eneo hilo.
Hata hivyo, juhudi za kumtafuta mtendaji huyo kwa ajili ya ufafanuzi hazikufanikiwa baada ya kufika ofisini kwake na kuelezwa kuwa hayupo. lakini kupitia maongezi ya njia ya simu, alisema kuwa yupo kikazi ziarani