Kagera Community Radio

Kagera kuungwa katika gridi ya taifa ya umeme

August 26, 2025, 6:27 pm

Msongo wa umeme

Wiazara ya Nishati imesaini mikataba miwili ya mradi wa ujenzi wa  njia ya kusafirisha umeme kwa msongo wa kilovoti 220 kutoka Benako wilayani Ngara hadi Kyaka wilayani Missenyi utakaowezesha mkoa wa Kagera kuungwa katika gridi ya taifa ya umeme.

Na Anold Deogratias

Mkoa wa Kagera unatarajiwa kuungwa katika gridi ya taifa ya umeme kufuatia utiaji saini wa mikataba miwili ya mradi wa ujenzi wa  njia ya kusafirisha umeme kwa msongo wa kilovoti 220 kutoka Benako wilayani Ngara hadi Kyaka wilayani Missenyi na ujenzi wa kituo cha kupooza umeme cha Benako chenye msongo wa kilovoti 220/33.

Akizungumza wakati wa utiaji saini mikataba hiyo  Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Dkt. Doto Biteko ameushukuru uongozi wa shirika la umeme nchini (TANESCO) kwa kukamilisha taratibu za mikataba hiyo na kusainiwa na wakandarasi.

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nshati Dkt.Doto Biteko akizungumza katika hafla hiyo.

Aidha Dkt.Biteko ameuagiza uongozi wa TANESCO kuhakikisha unawalipa fidia kiasi cha shilingi bilioni 2.6 wananchi wote wanaotakiwa kupisha mradi ifikapo  Septemba 2025.

Sauti ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nshati Dkt.Doto Biteko

Naye mkuu wa mkoa Fatma Mwassa ameishukuru Serikali kwa hatua za kutekeleza miradi hiyo na kueeleza kuwa  kwa sasa mkoa wa Kagera unatumia umeme megawati 46. Megawati 31 kutoka Masaka Uganda, megawati 9 kutoka Kakagati Murongo na megawati 6 kutoka Nyakanazi  Biharamulo.

Mkuu wa mkoa wa Kagera Fatma Mwassa akizungumza katika hafla hiyo

Pia mkuu huyo wa mkoa ameongeza kuwa miradi hiyo itaufaisha mkoa wa Kagera kwa kuziunga Wilaya zote saba katika gridi ya taifa na umeme utakuwa wa uhakika, hivyo kuwanufaisha wazalishaji wakubwa kama kiwanda cha sukari Kagera na viwanda vingine vya kusindika zao la kahawa.

Miradi iliyosainiwa mikataba itagharimu kiasi cha shilingi bilioni 262.5 ikikamilika.