Kagera Community Radio

Hekari 289 zarejeshwa katika kijiji cha Igurwa

July 24, 2025, 11:46 pm

Baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Igurwa waliohudhuria mkutano wa hadhara. Picha na Anold Deogratias

Kijiji cha Igurwa kilichopo kata ya Igurwa wilayani Karagwe mkoani Kagera kimerejeshewa hekari 289 zilizokuwa limechukuliwa na mwananchi mmoja kwa njia isiyo halali.

Na Anold Deogratias

Mkuu wa Wilaya ya Karagwe mkoani Kagera Julius Laizer ametatua mgogoro wa ardhi baina ya kijiji cha Igurwa kata ya Igurwa na mwananchi mmoja uliodumu kwa miaka 9 na kurudisha hekari 289 za kijiji hicho.

Mkuu wa Wilaya ya Karagwe Julius Laizer

Akizungumza katika mkutano wa hadhara kijijini hapo, DC Laizer amewataka viongozi pamoja na wananchi kufuata taratibu za uuzaji na utoaji wa ardhi, ikiwemo kuwa na hatimiliki ya ardhi husika pamoja na kuidhinishwa na mkutano wa kijiji kwa ardhi ya kijiji.

Sauti ya Mkuu wa Wilaya ya Karagwe Julius Laizer

Aidha mkuu huyo wa wilaya amewataka viongozi wilayani humo kutotumia madaraka yao kuwanyanyasa wananchi na kuanzisha migogoro.

Awali akitoa ufafanuzi juu ya mgogoro huo, Afisa Ardhi Wilaya ya Karagwe Bw. Alex Japhet Mpunji amesema mwananchi huyo Salvator Karabamu aliuziwa hekari 351 mali ya kijiji na wananchi 9 kinyume cha sheria, hivyo baada ya maridhiano mwananchi huyo amebakiziwa hekari 59 na hekari 289.98 zimerudi kwenye kijiji.

Sauti ya Afisa Ardhi Wilaya ya Karagwe Bw. Alex Japhet Mpunji

Nao baadhi ya wananchi wa kijiji cha Igurwa Elizabeth Damiani, Livnus Method na Telesphor Maganga wameshukuru Mkuu wa Wilaya kwa namna alivyoutatua mgogoro huo kwa njia ya maridhiano na kuomba kuendelea kutumia njia hiyo ili kupunguza kesi mahakamani na kutotumia muda mrefu.

Sauti ya wananchi wa kijiji cha Igurwa

Mgogoro baina ya uongozi wa kijiji cha Igurwa na mwananchi huyo ulianza mwaka 2016, baada ya uongozi huo kudai ardhi hiyo aliyouziwa kinyume cha sheria.

Baadhi ya wananchi wa kijiji cha Igurwa walioudhuria mkutano wa hadhara