Kagera Community Radio

Halmashauri ya Bukoba yazindua zoezi la chanjo ya kuku

July 2, 2025, 2:13 am

Kaimu mkurugenzi wa halmashauri ya Bukoba Julius Shulla akizindua zoezi la chanjo ya kuku

Halmashauri ya wilaya ya Bukoba mkoani Kagera imezindua zoezi la chanjo ya kuku, huku wataalam wa mifugo ngazi ya kata wakitakiwa kufanya kazi kwa uweledi na kwa muda uliopangwa.

Na Anold Deogratias

Wataalamu wa mifugo ngazi ya kata wataohusika katika utoaji wa chanjo ya kuku katika halmashauri ya wilaya ya Bukoba mkoani Kagera wametakiwa kufanya kazi hiyo kwa uweledi na kwa muda uliopangwa ili kuhakikisha lengo la serikali la uchanjaji wa mifugo linatimia.

Wito huo umetolewa na kaimu mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Bukoba, Ndugu Julius Shulla, wakati wa uzinduzi wa zoezi la ugawaji wa chanjo ya kuku kwa wataalamu wa mifugo ngazi ya kata, katika hafla iliyofanyika tarehe 1 Julai 2025, katika makao makuu ya halmashauri hiyo.

Kaimu mkurugenzi wa halmashauri ya Bukoba Julius Shulla akikabidhi chanjo ya kuku kwa mmoja wa wataalam wa mifugo

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Ndugu Shulla alieleza kuwa chanjo hiyo imetolewa bure na Serikali kupitia wizara ya mifugo na uvuvi, kwa lengo la kuwalinda wafugaji dhidi ya hasara zinazotokana na magonjwa ya kuku, huku akisisitiza kuwa zoezi la chanjo litafanyika kuanzia Julai 1 hadi Julai 15, 2025, na kila afisa mifugo anatakiwa kutekeleza jukumu hilo kwa uaminifu na weledi mkubwa.

Sauti ya Julius Shulla kaimu mkurugenzi halmashauri ya wilaya ya Bukoba

Chanjo hiyo aina ya tatu moja imelenga kuwakinga kuku na bata dhidi ya magonjwa hatari ikiwemo mdondo (Newcastle disease), Ndui (Fowl Pox), na Mafua ya kuku (Infectious Coryza), ambayo yamekuwa yakisababisha vifo vya ndege na hasara kwa wafugaji nchini.

Wataalamu wa mifugo wakiwa na chanjo ya kuku

Katika hatua nyingine wananchi na wafugaji halmashauri ya Bukoba wametakiwa kutoa ushrikiano kwa wataalam hao ili kufanikisha zoezi hilo.

Zoezi hili ni sehemu ya kampeni ya kitaifa inayotekelezwa katika halmashauri zote nchini, na linatarajiwa kuleta matokeo chanya katika kuinua afya ya mifugo na kipato cha wafugaji.

Wataalam wa mifugo halmashauri ya Bukoba wakipokea maelekezo kutoka kwa kaimu mkurugenzi Julius Shulla