Buha FM Radio

Wafurika kambi ya madaktari bingwa Hospitali ya Rufaa Kabanga

13 April 2026, 9:35 pm

Baadhi ya wananchi wakisubiri huduma za madaktari bingwa katika hospitali ya rufaa Kabanga. Picha na Sharifat Shinji.

Wananchi mkoani Kigoma wafurahia huduma za madaktari bingwa katika Hospitali ya Rufaa Kabanga.

Na Sharifat Shinji

Wananchi wa Wilaya ya Kasulu na Mkoa wa Kigoma kwa ujumla wamejitokeza kwa wingi katika hospitali ya rufaa Kabanga kwa ajili ya kupata huduma za kibingwa ambazo zinaendeshwa hospitalini hapo kwa wiki nzima.

Baadhi ya wananchi akiwemo Lameck Nzabuka na Gladys Emmanuel wameeleza furaha yao ya kufika katika hospitali hiyo kwa ajili ya kupata huduma za kibingwa huku wakipongeza zoezi zima la utoaji huduma kwa wagonjwa wanaofika kupata matibu hospitalini hapo.

Suuti ya Lameck Nzabuka na Gladys Emmanuel.
Mgonjwa akipata huduma kutoka kwa Daktari wa hospitali ya rufaa Kabanga. Picha na Sharifat Shinji.

Aidha kwa upande wake Kilian Wiliam  amemepongeza jitihada za hospitali hiyo kuleta kambi ya madaktari bingwa wa kada mbalimbali kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wenye changamoto za kiafya huku akiomba hospitali kutoa kipaumbele kwa wagonjwa wanaotoka nje ya Wilaya ya Kasulu na mkoa wa Kigoma  ili wapate huduma hizo mapema.

“Kwanza tuipongeze hospitali kwa kuleta madaktari bingwa ambao watasaidia wananchi kuwatibu magonjwa mbalimbali kama tulivyosikia kwenye tangazo bila shaka tutapata huduma nzuri na kama tunavyoona watu wamekuja kwa wingi kupata huduma hii iliyotangazwa na hospitali.” Amesema Wiliamu.

Sauti ya Kilian Wiliam.

Hospitali ya rufaa Kabanga imeanza kambi ya madaktari bingwa leo April 13 ambapo inatarajiwa kutamatika April 17, 2026 lengo likiwa ni kutoa huduma kwa wananchi wote wa mkoa wa Kigoma na maeneo jirani wenye changamoto mbalimbali za magonjwa yanayohitaji usaidizi wa madaktari bingwa wa kada mbalimbali.

Wananchi wakiwa kwenye foleni ya kupata huduma ya kuonana na madaktari bingwa. Picha na Sharifat Shinji.