Buha FM Radio

MEO’s Kasulu warudisha kwa watoto wenye mahitaji maalum

November 30, 2025, 10:36 pm

Baadhi ya wanajumuiya ya watendaji wa serikali za mitaa (MEO`s) Halmashauri ya Mji Kasulu wakiwa kwenye picha na watoto wa kituo cha Center of Hope  kinacholea watoto wenye mahitaji maalumu pamoja na baadhi ya misaada waliyoitoa katika kituo hicho. Picha na Herbeth Barayata.

Kituo cha kulelea watoto wenye mahitaji maalumu cha Center of Hope kimepokea misaada kutoka jumuiya ya watendaji wa serikali za mitaa (MEO`s) Halmashauri ya Mji Kasulu mkoani Kigoma ikiwa ni sehemu ya faraja kwa watoto hao kutokana na mahitaji waliyonayo wanapokuwa katika kituoni hicho.

Na; Paulina Majaliwa

Jumuiya ya watendaji wa serikali za mitaa (MEO`s) Halmashauri ya Mji Kasulu mkoani Kigoma wametoa msaada katika kituo cha Center of Hope  kinacholea watoto wenye mahitaji maalumu katika  Halmashauri hiyo.

Akizungumza kituoni hapo  kwa niaba ya watendaji  hao Afisa mtendaji ,mtaa wa Kanazi kata ya Luhita na  mwenyekiti wa watendaji wa mitaa Kasulu mji Leonard  Yohana amesema  wadau mbalimbali wanapaswa kuwa sehemu ya faraja kwa watoto hao kutokana na mahitaji waliyonayo wanapokuwa kituoni hapo.

Sauti ya afisa mtendaji wa mtaa wa kanazi kata ya Luhita.
Afisa mtendaji ,mtaa wa Kanazi kata ya Luhita na  mwenyekiti wa watendaji wa mitaa Kasulu mji Leonard  Yohana akieleza lengo la kutoa misaada hiyo. Picha na Herbeth Barayata.

Aidha amewataka watendaji wa mitaa wilayani humo kuwasaidia watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi ili kujenga jamii yenye watu wanaowajibika ndani ya nchi.

“Niwaombe watendaji wa mitaa tuwe na utaratibu wa kujua mazingira ya watoto wanaotuzunguka katika mazingira yetu kwasababu sisi ndio tunaishi nao karibu hivyo tuwasaidie watoto hawa” Amesema Leonard.

Kwa upande wake mkurugenzi wa shirika la corrective calling International, meneja wa kituo cha Centre of hope na mwanasheria mkuu wa kituo hicho Rebeka Rocky amesema shirika hilo linajihusisha na uokozi,utambuzi na kusaidia watoto wenye mahitaji maalumu kwa lengo la ulinzi wa mtoto.

Sauti ya meneja wa kituo cha Centre of hope Rebeka Rocky.
Baadhi ya wanajumuiya ya watendaji wa serikali za mitaa (MEO`s) Halmashauri ya Mji Kasulu wakiwa kwenye picha na watoto wa kituo cha Center of Hope  kinacholea watoto wenye mahitaji maalumu pamoja na baadhi ya misaada waliyoitoa katika kituo hicho. Picha na Herbeth Barayata.

Katika hatua nyingine amebainisha kuwa  kituo kinapokea watoto yatima na watoto wanaoishi katika mazingira magumu ambapo  mpaka sasa kuna waatoto 48, baadhi yao wapo katika hatua ya awali,shule za msingi,sekondari na vyuo.

Sauti ya meneja wa kituo cha Centre of hope Rebeka Rocky.

Naye kaimu mkuu wa wilaya ya kasulu Ibrahimu Mwangarume  amewataka watendaji wa serikali za mitaa halmashauri ya mji kasulu kutumia mitandao ya kijamii kwa maslahi ya kujenga taifa na sio kutumia mitandao ya kijamii kuleta taharuki katika mitaa wanayoongoza.

Sauti ya kaimu mkuu wa wilaya ya kasulu Ibrahimu Mwangarume.

Jumuiya ya watendaji wa serikali za mitaa Halmashauri ya mji Kasulu (MEOS) imeanzishwa mwaka 2024  ikiwa na malengo ya kuwaleta pamoja katika shughuli za kiutendaji ,kusaidiana katika shida na raha,kuwa chanzo cha ufumbuzi wa changamoto za watendaji,kupeleka mawazo,mapendekezo  na changamoto katika mamlaka za juu pamoja na kuimarisha ujamaa na kusaidiana.