Buha FM Radio

Mwenge wa Uhuru kutua Kasulu Septemba 17-18

September 8, 2025, 4:12 pm

Mkuu wa Wilaya ya Kasulu Mhe. Kanal Isack Mwakisu akiwa kwenye picha ya pamoja na waendesha Baiskeli na wadau wa Mbio za Mwenge wilayani Kasulu. Picha na Sharifat Shinji.

Mhe. Kanal Isack Mwakisu amewaomba wadau na wananchi kujitokeza katika mapokezi ya mbio za mwenge wa Uhuru mwaka 2025 siku ya tarehe 17 ambapo utapokelewa katika Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu na tarehe 18 mwezi huu katika Halmashauri ya Mji Kasulu.

Na; Sharifat Shinji

Mkuu wa Wilaya ya Kasulu Mhe. Kanal Isack Mwakisu amewaomba wananchi wa Wilaya hiyo kujitokeza katika mapokezi ya Mwenge wa Uhuru unaotarajiwa kufika katika wilaya hiyo Septemba 17 mwaka huu.

Ameyasema hayo siku ya Jumamosi Septemba 6, wakati wa ufunguzi wa Bonanza lililofanyika katika uwanja wa Kiganamo katika Halmashauri ya Mji Kasulu na kusema mwenge utapitia miradi yote ya Wilaya ya Kasulu.

Sauti ya Mhe. Kanal Isack Mwakisu akizungumzia ujio wa Mwenge wa Uhuru 2025 katika Wilaya ya Kasulu.
Mhe. Mkuu wa Wilaya ya Kasulu Kanal Isack Mwakisu akikabidhi zawadi kwa washindi wa mechi ya Bonanza la maandalizi ya kuupokea mwenge wa Uhuru 2025. Picha na Sharifat Shinji.

Aidha Mwakisu amewahamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kuushangilia mwenge wa Uhuru popote utakapopita kuzindua miradi ya maendeleo katika Halmashauri zote za Wilaya ya Kasulu.

“Niwaombe sana wananchi tarehe 17 mwenge utaingia katika Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu utatembelea miradi yote katika Wilaya na kukesha katika viwanja vya Nyamnyusi kasha tarehe 18 tutaupokea katika Halmashauri ya Mji Kasulu hivyo tujitokeze kwa wingi kuupokea mwenge wetu wa Uhuru kisha kuushangilia popote utakapopita” Amesema Mwakisu.

Kwa upande wake Katibu Tawala Wilaya ya Kasulu na Mratibu wa Bonanza hilo Bi Telesia Mtewele amesema lengo la kuandaa Bonanza ni kuhamasisha wananchi kujitokeza katika mapokezi ya mbio Za Mwenge ili Wilaya iweze kufanya vizuri Kimkoa na kitaifa kwa Ujumla.

Sauti ya Katibu Tawala na Mratibu wa Bonanza la kuukalibisha Mwenge wa Uhuru Bi Telesia Mtewele.
Katibu Tawala Wilaya ya Kasulu akisungumza na wananchi kuhusu umhimu wa Bonanza la mapokezi ya mbio za Mwenge wa Uhuru 2025. Picha na Sharifat Shinji.

Katika hatua nyingine Mwl. Elisha ambaye ni mdau na mwandalizi wa mbio za mwenge Katika Wilaya ya Kasulu amesema mwenge wa uhuru unakuja kumulika miradi yote iliyopo katika Wilaya ya kasulu huku akiwahamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi katika mapokezi pamoja na kushiriki uchaguzi mkuu mwaka huu.

Sauti ya Mwl. Elisha mudau wa Mbio za mwenge na mshindi wa shindano la kukimbiza kuku kwa upande wa wanaume katika Bonanza.
Katibu Tawala Wilaya ya Kasulu na Mkuu wa Wilaya ya Kasulu wakiwa na wadau mbalimbali wa Mbio za Mwenge wa Uhuru 2025. Picha na Sharifat Shinji

Mwenge wa Uhuru 2025 unatarajiwa kuwasili katika Wilaya ya Kasulu mnamo tarehe 17 ambapo utaanzia Halmashauri ya wilaya ya Kasulu na tarehe 18 utawasili katika Halmashauri ya Mji Kasulu na kufanya ukaguzi wa Miradi yote iliyopo katika Halmashauri ya Mji Kasulu.