Buha FM Radio

Mapishi ya mwanaume kuondoa utapiamlo katika familia

May 12, 2025, 7:37 pm

Pichani ni baadhi ya vyakula tofautitofauti vinavyounda mlo kamili. Picha na Paulina Majaliwa.

“Wanaume simamieni chakula katika familia ili watoto wenu wawe na afya bora kwa sababu watoto wanakua kila siku  na wanahitaji kula chakula chenye virutubishi vyote ili wakue vizuri” Amesema Kimambo.

Na: Paulina Majaliwa

Wanaume katika Halmashauri ya Mji Kasulu wameshauriwa kushirikiana na wenza wao katika uandaaji wa chakula  ili kuepukana na utapiamlo na magonjwa kwa watoto na familia kwa ujumla.

Hayo yamesemwa na Afisa Lishe wa Shirika la Kilimo na Chakula Duniani FAO Bi. Stella Kimambo katika maadhimisho ya miaka 80 ya FAO yaliyofanyika kata ya Nyasha katika halmashauri hiyo mkoani Kigoma ambapo amesema ushiriki wa wanaume katika kuandaa chakula  itasaidia  ulaji wa mlo kamili katika familia.

Sauti ya afisa lishe FAO Bi. Stella Kimambo.

Aidha amesema kuwa ili kujenga jamii yenye afya bora wanaume pia wana wajibu wa kushiriki  katika kuandaa na kupangilia ulaji wa chakula bora katika jamii ili kuimarisha afya kwa familia.

“Nawasihi wanaume simamieni chakula katika familia ili watoto wenu wawe na afya bora kwa sababu watoto wanakua kila siku na wanahitaji kula chakula chenye virutubishi vyote ili wakue vizuri” amesema Stella Kimambo.

Pichani baadhi ya washiriki wa kiume wamafunzo ya lishe bora katika halmashauri ya Mji Kasulu. Picha na Paulina Majaliwa.

Kwa upande wake afisa lishe katika halmashauri ya Mji Kasulu Ndg. John Sabatele amesema kuwa jamii inatakiwa kuepuka ulaji wa vyakula vyenye sukari kwa wingi na mafuta kwa wingi ili kuepukana na magonjwa yasiyoambukizwa kama vile kisukari, shinikizo la damu na magonjwa ya mishipa.

Sauti ya afisa lishe Kasulu Ndg. John Sabatele.

Nao baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo wamesema kuwa wataendelea kutumia elimu waliyoipata kupitia mafunzo hayo ya lishe kutoka katika shirika la FAO pia wamesema watakuwa mabalozi kwa wananchi wengine ambao hawajabahatika kupata elimu hiyo.

Sauti ya washiriki wa mafunzo ya Lishe bora.

Chakula bora ni muhimu kwa binadamu kwani huupatia mwili nishatti,lishe na virutubishi mbalimbali ili kuuwezesha mwili kufanya kazi kwa ufanisi hivyo ni vyema kuzingatia ulaji bora wa chakula ili mwili uweze kupata mahitaji yote ya lishe.

Picha ni washiriki wa mafunzo ya lishe na chakula bora katika familia wakiendelea na mafunzo. Picha na Paulina Majaliwa.