Buha FM Radio
Buha FM Radio
February 11, 2026, 8:46 am

Maafisa usafirishaji katika Wilaya ya Kasulu wapewa elimu ya kufuata ili kupata leseni za udereva huku wakitaja ugumu wa maisha ni sababu ya kutokufuatilia masuala ya leseni.
Na: Sharifat Shinji
Maafisa Usafirishaji abiria katika Wilaya ya Kasulu Mkoani Kigoma wametakiwa kufuata nia bora za kupata leseni ya udereva ili kupunguza changamoto za ajali barabarani pamoja na kuepuka usumbufu wa vyombo vya usalama.
Maagizo hayo ameyatoa Mrakibu wa Polisi kitengo cha Usalama Barabarani wilayani humo SP Patrick Damas wakati akizungumza na waendesha vyombo vya moto na kuwasisitiza umuhimu wa kuwa na leseni ya udereva.

Aidha amewaomba viongozi wa vijiwe vya maafisa hao kuhakikisha wanasimamia sheria walizojiwekea ikiwemo kufuata taratibu za kisheria ili kudhibiti makosa ambayo baadhi ya waendesha vyombo vya moto wanayafanya.
Kwa upande wao baadhi ya maafisa na waendesha vyombo vya moto maarufu bodaboda wameshukuru na kueleza namna walivyopokea maelekezo ya mkuu wa usalama juu ya kufuata taratibu za kiusalama barabarani.

Kwa mujibu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri Ardhini (LATRA) katika kipindi cha mwaka 2023/2024 mamlaka ilitoa jumla ya leseni 46,146 za pikipiki, ikiwa ni ongezeko la asilimia 44.5 ikilinganishwa na leseni 31,937 zilizotolewa katika kipindi kama hicho cha mwaka wa fedha 2022/2023.
