Kagera Community Radio
Kagera Community Radio
July 16, 2025, 5:58 pm

Wahamiaji haramu 52 kutoka nchi ya Burundi wamekamatwa wilayani Ngara mkoani Kagera wakiwa wanasafirishwa kuelekea jijini Mwanza.
Na Anold Deogratias
Idara ya Uhamiaji kwa kushirikiana na jeshi la polisi mkoa wa Kagera wamefanikiwa kuwakamata wahamiaji haramu 52 kutoka nchi ya Burundi walioingia nchini bila kufuata utarabibu wakielekea jijini Mwanza.

Akiongea na waandishi wa habari wilayani Ngara mkoani Kagera, Afisa Uhamiaji Mkoa wa Kagera Kamishina Msaidizi wa Uhamiaji Petro Malima amesema kuwa watu hao wamekamatwa wakiwa kwenye gari lenye namba za usajili T692 EGU mali ya King Msukuma, kufuatia oparesheni inayoendeela ya kuwaondoa wahamiaji haramu mkoani Kagera.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera Blassius Chatanda amesema kuwa uwepo wa watu wanaoingia nchini bila utaratibu kunaweza kusababisha kuingia kwa watu ambao hawana nia njema na kusababisha uvunjifu wa amani.

Aidha Kamanda Chatanda, amewataka wamiliki wa vyombo vya moto kuhakikisha wanajiepusha na kufanya biashara ya wahamiaji haramu hali inayoweza kusababisha kutaifishwa kwa vyombo vyao.
Ikumbukwe wiki iliyopita Idara ya Uhamiaji iliwarudisha wahamiaji haramu 800 kwenye maitaifa yao kutoka wilaya mbalimbali za mkoa wa Kagera huku zikiwa zimetolewa siku saba kwa wahamiaji hao kujisalimisha na kurejea makwao.