Storm FM

Mgogoro wa wachimbaji wa dhahabu wamalizika

13 May 2021, 9:42 am

Wachimbaji wadogo wa madini ya dhahabu katika wilaya ya Mbogwe Mkoani Geita wameipongeza serikali kupitia wizara ya madini kwa kumaliza mgogoro wa wachimbaji katika mgodi wa Nyakafuru.

Wakizungumza na Storm FM siku chache baada ya waziri wa madini Mhe, Dotto Biteko kufika na kumaliza mgogoro uliyodumu kwa kipindi kirefu baadhi ya wachimbaji wadogo wa madini ya dhahabu wamesema hatua hiyo itasaidia kuongeza uzalishaji tofauti na hapo awali.

Kwa upande wake Diwani wa kata ya Nyakafuru Bw Paul Edward amesema mgogoro uliyokuwepo katika eneo hilo ni kati ya watu waliyokuwa wakidai kuwa ndio wamiliki halali wa mashamba kushindwa kuelewana na kikundi kilichopewa dhamana ya kusimamia mgodi huo na serikali ya wilaya ya mbogwe.

Akizungumzia hatua hiyo Mbunge wa Jimbo la Mbogwe Nikodemas Maganga amesema migogoro hiyo imeathiri shughuli za uchimbaji wa madini katika mgodi huo kwa kipindi kirefu nakwamba kumalizika kwa changamoto hiyo kutatoa fursa kwa watu wengi kufanya kazi katika eneo hilo.