Sibuka FM

Maswa: Wakazi wa mji wa Malampaka walalamikia mgao wa maji

30 March 2023, 5:39 pm

Na Alex.F.Sayi

Wakazi zaidi ya elfu ishirini na nne wa Mji wa Malampaka Wilayani Maswa Mkoani Simiyu,wanakabiliwa na adha  ya mgao wa maji unaotokana na upungufu wa maji safi na salama mjini hapo.

Akizungumza na Sibuka fm redio Diwani wa Kata hiyo,Renatus Mashala amesema kuwa hali ya upatikanaji wa Maji Katani hapo niwashida kutokana na uwepo wa Mgao unaoendelea kwa sasa.

“Maji kwa sasa tunayapata kwa asilimia (45%) niyamgao na kata yangu inakaya elfu tatu ukiweka na ongezeko la watu kutokana na Ujenzi wa (SGR)kunakuwa na wakazi zaidi ya elfu (24) unapoweka mgao wa maji kwenye idadi kubwa ya watu kama hawa maana yake unapunguza hata uzalishaji na mzunguko wa biashara hasa kwa mama lishe ambao wanategemea maji ili kuendesha shughuli zao.”Amesema Mashala.

Diwani huyo amesema kuwa ukosefu wa Maji Mjini hapo umewalazimu wakazi hao kununua Maji kwa (Sh.500) kwa Dumu moja la lita Ishirini.

“Kwa sasa baadhi ya wananchi wanalazimika kununua Maji kwa (Sh.500),ingawa tunaishukuru Serikali kwa kutuletea Mradi Mpya utakao saidia upatikanaji wa Maji kwa asilimia (75%)kama utasimamiwa vizuri.”Amesema Diwani.

Elizabeth Clement ni mkazi wa Malampaka amesema kuwa uhaba  wa Maji unasumbua sana Wanawake yakikatika wanalazimika kuamka saa,9 za usiku kufuata Maji mtoni umbali wa kilomita mbili  hali ambayo imepelekea kuwa na migogoro mingi ya ndoa kutoka kwa Waume zao ambao wamekuwa wakilalamikia kukosa tendo la ndoa kwa nyakati za alfajiri .

“Ukosefu wa maji mjini hapa umepelekea migogoro mingi ya ndoa kutoka kwa waume zetu ambao wanadai kukosa tendo la ndoa kwa wakati huo ,maana maji tunalazimika kufuata umbali wa kilomita 2 mtoni wakati mwingine kurudi inachukua muda hadi saa mbili asubuhi” Amesema Elizabeth

Naye, Bi. Mariam John Mkazi wa Malampaka amesema kuwa kumekuwa na mgao wa Maji wa hadi siku tatu kwa kila kitongoji hivyo kuwalazimu kununua Maji,wakati mwingine kulazimika kufuata Maji mtoni ambayo siyo safi na salama kwa matumizi ya binadamu.

Akizungumzia suala la upatikanaji wa Maji katika Mji wa Malampaka kaimu mkurugenzi wa(Mauwasa) Mhandisi wa Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Maswa(Mauwasa)Mhandisi Raphael Mwita, amesema kuwa kwa sasa wanaendelea na Ujenzi wa Mradi wa Maji wa dharura ili kuendana na kasi ya ukuaji wa Mji huo.

“Tumefunga mkataba na Mkandarasi SAVANNA ESAP CO LTD wa   Mwanza kwa zaidi ya (Sh.Millioni 68.1)kwa kazi ya kuchimba kisima kirefu kimoja,na tumefunga mkataba na Mkandarasi DATTI CONSTRUCTION LTD wa  Mwanza kwa zaidi ya (Sh.million 281.8)kwa kazi ya ujenzi wa tank la kuhifadhi Maji lita laki moja na ujenzi wa mfumo wa kusambazia maji Malampaka wa Km 3.”Amesema Mhandisi Mwita.