Radio Jamii Kilosa

Jamii yasisitizwa kuendelea kuchukua tahadhari .

4 March 2021, 9:51 am

Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Adam Mgoyi

Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Adam Mgoyi ameonyesha kuridhishwa kwake na utendaji kazi wa kitengo kinachosimamia utekelezaji wa afua mbalimbali katika kitengo cha magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele kwa namna ambavyo kimekuwa kikifanya majukumu yake na kutoa mrejesho chanya katika utekelezaji wake kwani kimekuwa chachu ya mabadiliko katika jamii ambapo kwa zaidi ya asilimia 75 matokeo ya utekelezaji ni mazuri huku akitaka na vitengo vingine vilivyoko chini ya idara ya afya kuongeza juhudi ili kuwa na mabadiliko chanya kwenye jamii.

Akitoa pongezi hizo Machi 3 mwaka huu Mgoyi amesisitiza jamii kiujumla kuendelea kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa wa corona kwa kuzingatia maelekezo yote yanayotolewa na wataalam wa afya kwani misiba katikati ya jamii imekuwa mingi hivyo ni vema jamii ikaendelea kupata elimu na kuchukua tahadhari ikiwemo kuvaa barakoa na tahadhari nyinginezo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya kilosa Asajile Lucas Mwambambale .

Aidha Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa Asajile Mwambambale amewataka viongozi wote wa vitengo mbalimbali vilivyoko katika idara kuwajibika kwa sehemu yao na kufanya kazi zenye kuleta tija badala kumwachia majukumu yake mkuu wa Idara au Mkurugenzi au Mkuu wa Wilaya kwani kila mtu anao wajibu wa kuwajibika na kujitoa kwa dhati kufanya kazi katika eneo lake kikamilifu kwa lengo la kuleta matokeo chanya.

Pamoja na hayo amesema Halmashauri imejipanga kwa dhati kufanya mabadiliko makubwa katika sekta mbalimbali hususani sekta ya afya ambapo suala la lishe litapewa kipaumbele kwa umuhimu wake ili kuwa na jamii yenye afya bora huku akikitaka kitengo kinachoshughulika na suala la utoaji dawa mashuleni kwa ajili ya wanafunzi kutoa ratiba mapema ili idara zinazohusika ziweze kuweka taratibu zinazostahiki ikiwemo upatikanaji wa chakula mashuleni.

Mratibu wa magongwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele Wilaya kilosa Rosemary Nguruwe .

Naye Mratibu wa magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele Wilaya Rosemary Nguruwe  amesema kuwa kwa asilimia kubwa shughuli zilizopangwa zimefanyika huku akisema kuwa zaidi ya asilimia 95 ya fedha zimetumika kama ilivyopangwa, lakini pia ushirikiano mzuri kati ya miradi mingine ,kuongezeka kwa wanafunzi wanaomeza dawa kila mwaka pamoja na ushiriki mzuri wa wadau mbalimbali katika shughuli za NTDs wakiwemo viongozi wa dini na Chama Tawala (CCM) huku baadhi ya changamoto zilizojitokeza ni shule nyingi kutokuwa na chakula, ushiriki mdogo wa viongozi hasa katika vitongoji, utoaji wa  fedha kuchukua muda mrefu, kutofanyika kwa zoezi kwenye jamii mwaka 2020 na mawasiliano hafifu kwa baadhi ya ofisi.