Radio Fadhila

MBUNGE wa Jimbo la Masasi, Geofrey Mwambe ametoa vifaa ya Michezo Klabu ya mpira wa miguu ya Mkuti Makerti ya mjini Masasi

4 March 2021, 4:07 AM

MBUNGE wa Jimbo la Masasi, Geofrey Mwambe ambaye pia ni Waziri wa Viwanda na Biashara amewapatia vifaa mbalimbali vya Michezo Klabu ya mpira wa miguu ya Mkuti Makerti ya mjini Masasi ambapo Timu hiyo kwa sasa ndio imefanikiwa kuwa Bingwa wa Mkoa wa Mtwara na inakwenda kushiriki mashindano ya mabingwa wa mkoa kwa kituo cha mkoa wa Lindi mashindano ambayo yanatarajia kuanza mwishoni mwa wiki hii mkoa Lindi. Baadhi ya vifaa hivyo ambavyo vimekabidhiwa leo Machi, 3, 2021 na Katibu wa Chama Cha Mapinduzi( CCM) wilaya ya Masasi Zainabu Chinowa kwa niaba ya Mbunge huyo na kupokelewa na viongozi wa Timu hiyo ni jezi pea mbili, mipara 5 , koni kwa ajili ya mazoezi. Akitoa ujumbe wa Mbunge kuhusu kutoa vifaa hivyo, katibu wa Mbunge, Imani Mkumbo amesema Mbunge huyo ameamua kutoa vifaa hivyo kwa kuwa anathamini michezo na kwamba Timu hiyo kuwa Bingwa wa mkoa imeutangaza mkoa wa Mtwara. Amesema Ofisi ya Mbunge itashirikiana vema na viongozi , wadau na wapenzi wa Timu hiyo ili kuhakikisha inaenda kufanya vizuri katika mashindano hayo ya mabingwa wa mkoa kituo cha Lindi. Kwa upande wake, Mlezi wa Timu hiyo , Mahafuzi Saidi amesema kwa ya niaba ya uongozi wa Timu hiyo wanampongeza Mbunge huyo kwa kuwapatia vifaa hiyo na kwamba wanathamini mchango wake huo. Aidha, Mahafuzi ametoa wito kwa wadau wote mkoani Mtwara wakiwemo wabunge wa mkoa wa Mtwara kuendelea kuisaidia Timu hiyo kwa sababu kwa sasa Timu ambayo inawakilisha mkoa mzima wa Mtwara na sio Masasi pekee. Katibu huyo wa CCM wilaya ya Masasi ameweka wazi kuwa Chama hicho kitambua umuhimu wa michezo na kwamba hata ilani Chama hicho inasisitiza suala la michezo.