Pangani FM

Mpango kuapishwa kesho

30 March 2021, 6:41 pm

Makamu wa Rais Mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Mpango kesho tarehe 31 Machi, 2021 ataapishwa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Hafla ya kuapishwa kwa Dkt. Mpango itafanyika Ikulu, Chamwino Mkoani Dodoma kuanzia saa 9:00 alasiri.

Dkt. Mpango ataapishwa kushika wadhifa huo baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan kuwasilisha mapendekezo ya jina la Dkt. Philip Mpango kuwa Makamu wa Rais katika Kikao Maalum cha Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi na baadaye jina hilo kuwasilishwa Bungeni na kuthibitishwa kwa kura 363 sawa na asilimia 100 ya kura zote zilizopigwa.