Pangani FM

Zoezi la kuokoa mwili wa aliyetumbukia ‘shimo la mreno’ limesimama.

12 March 2021, 11:48 pm

Mtu mmoja anasadikiwa kufariki dunia baada ya kutumbukia katika shimo lijulikanalo kama Shimo la  Mreno lililopo katika kijiji cha jaira kata ya madanga hapa wilayani pangani Mkoani Tanga.

PANGANI FM imefika katika eneo hilo na kushuhudia jitihada mbalimbali za kuokoa mwili huo  zikiendelea  leo ijumaa bila mafanikio huku zoezi hilo likitarajiwa  kuendelea tena kesho jumamosi.

Akizungumza na wananchi waliojitokeza kushudhudia zoezi hilo katibu tawala wilaya ya pangani MWALIMU HASSAN NYANGE amesema kuwa wamefika eneo hilo baada ya kupata taarifa kutoka kwa uongozi wa kijiji hicho.

‘naomba niwape pole kwa jambo hili ambalo limemkuta ndugu yetu na niwashukuru viongozi wa vijiji ambao walitupa taarifa mapema na mara baada ya kutupa taarifa ndipo tukafika katika eneo la tukio tukaona kwa sisi hatutaweza kufanya lolote ndipo tulipowasiliana na jeshi la uokoaji kutoka mkoani”

Amesema DAS Pangani

Kwa upande wake kamanda wa zimamoto mkoa wa TANGA BI FATMA NGENYA ameelezea jitihada walizozifanya mara baada ya kupokea taarifa.

kwanza nitoa pole kwa hili ambalo limetutokea la kumpoteza mpendwa wetu kwenye hilo shimo na mara baada ya kupata taarifa hizi nmekuja na timu ya wataalamu kwa ajili ya kufanya uokozi wa mpendwa wetu ambae tumempoteza ila kutokana na kanuni na sheria na taratibu za nchi zinatukataza kufanya kazi usiku ila kutokana tumeshakagua eneo husika  lakini sasa haina kutokana na muda kwenda haina budi kuweza kufuata taratibu za nchi na tutaendelea tena kesho asubuhi

Amesema Bi Fatma

Wenyeji wa kijiji cha Madanga wameeleza kuwa shimo hilo lilikuwepo tangu enzi za mkoloni na hakuna taarifa kamili ya kina cha shimo hilo wala kilichopo ndani yake.