Pangani FM

Viwanda Mkoani Tanga vyatakiwa kuzingatia Sheria ya Mazingira.

22 February 2021, 8:14 pm

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Rais Muungano na Mazingira, Mh Ummy Mwalimu leo amefanya ziara katika jiji la Tanga ambapo amehimiza utunzaji wa Mazingira hususani kwa kuvitaka Viwanda kujiepusha na uchafuzi wa Mazingira.

Akziungumza katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tanga wakati alipokea Taarifa ya Hali ya Mazingira ya Mkoahuo na Hali ya Mazingira katika Halmashauri ya Jiji la Tanga,amedai kuwa pamoja na mengine taarifa hizo pia zimeonyesha uwepo uwepo wa uchafuzi wa Mazingira kutoka viwanda vya Saruji na Chokaa vilivyopo Jijini Tanga.

Pia Waziri Ummy amesema kuwa akiwa Waziri wa Mazingira hatafungia viwanda bali atavisaidia ili kuhakikisha vinazingatia matakwa ya Sheria ya Mazingira kwa lengo la kulinda Mazingira na afya za watanzania.

katika hatua nyingine Mhe Ummy ametembelea kiwanda cha kuzalisha Chokaa cha Neelkath – Liemba ambapo amekutana na uongozi wa kiwanda hicho na kuzungumzia uwepo wa kero ya vumbi na moshi kwa wakazi wa eneo hilo.

Mh Ummy ameagiza NEMC, Afisa Mazingira wa Mkoa pamoja na wa Halmashauri ya Jiji la Tanga kusimamia kikamilifu Sheria ya Mazingira na kutoa msaada wa kitaalamu kwa Mwekezaji kuhusu utunzaji wa Mazingira na kuongeza kuwa Serikali haipo kwa ajili ya kufungia viwanda bali kuwasaidia kwa kuhakikisha uwekezaji wao pia unazingatia matakwa ya Sheria ya kutunza na kuhifadhi mazingira.

Aidha Waziri huyo amempongeza Mwekezaji anayefahamika kama Liemba kwa kuajiri Mtaalam wa Mazingira wa kudumu na kudai kuwa hatua hiyo inadhihirisha utayari wake wa kutunza mazingira na kumtaka ashirikiane na Wataalamu wa Mazingira wa Mkoa, Halmashauri.