Pangani FM

Wanaume watakiwa kuvunja ukimya vitendo vya Ukatili

5 February 2021, 1:45 pm

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima amewataka wanaume kutoa taarifa kwenye mamlaka husika kuhusu ukatili wanaofanyiwa ili kutokomeza matukio ya ukatili nchini.

Dkt. Gwajima ametoa kauli hiyo leo jijini Dodoma alipotoa tamko kuhusu Vitendo vya Ukatili katika jamii mbele ya waandishi wa habari.

Gwajima amesema vitendo vya ukatili vimezidi kuongezeka hapa nchini akitolea mifano mbalimbali iliyotokea hivi karibuni ya waanfamilia kufanyiana vitendo vya kikatili.

Amesema ukatili haufanywi kwa wanawake na watoto tu lakini hata kwa makundi mengine ikiwemo wanaume lakini wengi wao wamekuwa wakinakaa kimya.

“Wanaume msione aibu, muache kukaa kimya dhidi ya vitendo vya ukatili mnavyofanyiwa. Toeni taarifa mapema kwa mamlaka husika muweze kupata msaada ili kuzuia madhara zaidi kutokea” amesema Gwajima.

Amesema Mh Gwajima

Amezitaja sababu za ukatili huu ni pamoja na migogoro ya kifamilia ikiwemo kugombea mali, matatizo ya kisaikolojia na jamii kutotekeleza wajibu wake wa kutunza na kuimarisha ulinzi kuanzia ngazi ya familia.

Dkt Gwajima amesema Wizara itaendelea kuchukua jitihada zote kuhakikisha ukatili unatokomezwa kwa makundi yote, lakini jamii pia ina jukumu la kuwalinda makundi yote.

Aidha, amesema Wizara itaendelea kushughulikia mauaji ya wazee na kuwa haitorudi nyuma kupambana na ukatili wa aina yoyote ili nchi na mipaka yake ibaki salama kwa amani, upendo na kujiletea maendeleo.

Naye Afisa Ustawi Jamii Mkuu kutoka Wizara ya Afya, Amina Mafita amesema Wizara imejikita zaidi katika kuelimisha jamii kwa kuunda mabaraza kuanzia ngazi za vijiji na mitaa kwa lengo la kulinda makundi yote.