Orkonerei FM

Msaada watolewa kwa watoto yatima karatu Arusha

17 March 2022, 9:58 pm

Na Nyangusi ole sang’da Arusha,
Wanawake kutoka Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) kwa niaba ya wanawake wengine wa Taasisi zilizoko chini ya Wizara ya Maliasili na utalii leo tarehe 17 Machi, 2022 wametembelea kituo cha Watoto yatima cha Jesus life Ophan Centre kilichopo Tarafa ya Eyas Wilayani karatu Mkoani Arusha kwa lengo la kuwafariji na kuwapa msaada wa mahitaji mbalimbali kama sehemu ya kutoa kwa jamii.

Wanawake hao walioongozwa na Afisa Uhifadhi Mkuu-Ikolojia kutoka NCAA Bi. Flora Assey wameeleza kuwa lengo la ziara hiyo ni kuwafariji watoto waishio katika mazingira magumu na kuwafariji kwa kuwapatia mahitaji mbalimbali ikiwa ni muendelezo sherehe za maadhimisho ya siku ya Wanawake duniani.

“Tangu tarehe 5-8 machi wakati wa maadhimisho wa wanawake duniani tulishiriki katika shughuli mbalimbali ikiwepo uhamasishaji wa shughuli za Utalii wa ndani, Uhifadhi, upandaji miti pamoja na kutembelea kituo cha Watoto wenye mahitaji mbalimbali eneo la Mto Wambu Monduli mkoani Arusha, na leo tumetembelea kituo hiki kwa lengo la kufanya matendo ya huruma” aliongeza Flora Assey.

Mkurugezi wa kituo cha Jesus Ophan Deodata Telemla ameeleza kuwa kituo kilichoanza mwezi mei mwaka 2021 kina hadi sasa kina jumla ya watoto 23 ambapo ambapo waliowengi walifiwa na wazazi na wengine kutelekezwa na kukosa malezi na haki ya kwenda shule hivyo uanzishwaji wa kituo hicho unalenga kuwakusanya Watoto hao na kuwaweka pamoja na kuwasomesha kwa ajili ya kumimiza ndoto zao.

Vifaa vilivyokabidhiwa kwenye kituo ni pamoja na Magodoro 6, Mchele kilo 100, Sabuni, juisi, maharage, mafuta ya kupikia, chunvi na fedha taslimu kiasi cha shilingi laki nane (800,000)