Nuru FM

Zaidi ya Mafundi smart 1800 kukutana march 17 kupeana Fursa

16 March 2023, 12:01 pm

Miongoni Mwa mafundi watakaohudhuria kongamano la Fundi smart. Picha na Mpiga Picha wetu

Kongamano la Mafundi Smart lina lenga kuonesha fursa za ajira kwa kundi hilo na kukuza kipato chao.

Na Mwandishi wetu

ZAIDI ya mafundi wa aina mbalimbali 1800 wanatarajia kukutana pamoja katika kongamano kubwa litakalo fanyika Mjini Iringa lengo kubwa likiwa kupanua wigo wa ajira na kuongeza fursa kwenye kundi hilo muhimu kwenye jamii.

Meneja wa FundiSmart, Fabian Mwiga amesema kongamano hilo litafanyika Machi 17, 2023 katika ukumbi wa Masiti, Manispaa ya Iringa.

Kiuhalisia, mafundi ni kati ya kundi lililoachwa pembeni licha ya kuwa vitu vingi zinavyoizunguka dunia vinatokana na uwepo wa fundi.

 “Tunawakutanisha mafundi mbalimbali bila kujali aina ya ufundi wao, mpaka sasa tunao mafundi 1800 waliojiandikisha,” amesema Mwiga.

Mafundi smart wakiwa kazini

Amesema kwenye kongamano hilo mafundi watapata fursa ya kujua umuhimu na thamani ya kazi yao, elimu ya afya na bima, fedha, sheria, akiba na huduma bora kwa wateja.

“Sekta ya ufundi ni nyeti na mafundi wanazo ndoto zao, sasa wanaweza kufikia ndoto zao ikiwa tutawaonyesha mlango wa kupita, FundiSmart imekuja kwa ajili hiyo,” amesema Mwiga.

Amesema kwa sababu kundi hilo limekuwa likilalamikiwa zaidi na wateja hasa kwenye suala la uaminifu, elimu kuhusu sheria na huduma kwa wateja itawasaidia zaidi.

Kwa upande wao baadhi ya mafunzi wamesema hakuna siku waliketi pamoja na kutambuliwa kama sekta nyeti.

‘Hata tukifanya kazi mtu anakulipa atakavyo bila kujali kazi kubwa unayofanya, naamini hii ni fursa kwetu kutambua kazi yetu na kuipatia kipaumbele,” amesema.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Halima Dendego anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye kongamano hilo.