Nuru FM

MEYA: Tamko Mgomo Madereva Daladala Iringa

27 February 2023, 3:44 pm

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Iringa Ibrahimu Ngwada akizungumza kuhusu mgomo katika baraza la madiwani.Picha na Ashura Godwin

Kufuatia mgomo wa madereva daladala siku ya leo katika halmshauri ya manispaa ya Iringa, madereva wa pikipiki za miguu mitatu maarufu bajaj,wameelezwa kuwa sababu  ya mgomo  huo. 

Na Hawa Mohammed.

Akizungumza katika kikao cha baraza la madiwani manispaa ya Iringa Mstahiki Meya wa Halmashauri hiyo Ibrahimu Ngwada amewaomba madereva wa daladala kusitisha mgomo ambapo ameeleza kuwa madereva bajaj wamekua wakikiuka makubaliano ambayo yamefikiwa na kuleta vurugu kwa kuingia maeneo ambayo hawatakiwi kuingia au kupita.

Hakuna bajaj yoyote itakayoaachiwa pasipo  taarifa rasmi  kutoka ofisi ya Mstahiki Meya.

Aidha Meya amekiri kuwepo kwa mgongano wa kimaslahi baina ya daladala na bajaji, na kwamba halmashauri ilikaa vikao kadhaa na madereva daladala na bajaj ili kuweka mikakati ya kumaliza mgogoro huo ikiwa ni pamoja na kutengeneza barabara za pembeni kwa kiwango cha lami ili bajaj ziweze kupita jambo ambalo limetekelezwa na halmashauri.

Katika hatua nyingine Meya Ngwada amesema baraza la madiwani limepewa mamlaka kisheria ya kusimamia suala hilo na hivyo kuwataka bajaj kufuata utaratbu uliowekwa na kuwaagiza kitengo cha sheria na Idara ya biashara manispaa ya Iringa kukamata bajaji zote ambazo zinavunja sheria.

Meya amesema suala la bajaj kwa sasa litakua chini ya ofisi yake na kwamba hakuna bajaj yoyote itakayoaachiwa pasipo  taarifa rasmi  kutoka ofisi ya mstahiki Meya.

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Iringa Ibrahimu Ngwada akieleza kwa undani kuhusu kadhia hiyo.