Nuru FM

TMA yatahadhari mvua kubwa mikoa sita

14 January 2023, 7:55 am

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imetoa angalizo la uwepo wa mvua kubwa zinazoweza kunyesha hii leo Jumamosi Januari 14, 2023 katika maeneo machache ya mikoa ya Morogoro, Singida, Dodoma, Iringa, Njombe na Ruvuma.

 

TMA kupitia taarifa yake ya utabiri, imetaja athari zinazoweza kujitokeza kuwa ni pamoja na makazi ya raia kusombwa na maji, maeneo ya bondeni kuzingirwa na maji na kuchelewa kwa shughuli za usafirishaji na uchumi

Mapema hapo Jana, Januari 13, 2023 ziliripotiwa habari za uwepo wa taharuki kwa wakazi wa kata za Lukobe, Kihonda na Mkundi zilizopo katika Manispaa ya Morogoro, ambapo mafuriko yaliyakumba maeneo hayo kutokana na mvua kubwa kunyesha.

 

Wakiongea kwa nyakati tofauti, Wakazi wa maeneo hayo wamesema mvua hiyo ilianza kunyesha majira ya saa nane usiku hadi saa kumi na mbili asubuhi na kuleta madhara ya nyumba kuanguka, huku vitu mbalimbali vikisombwa na maji.