Nuru FM

Onesho La S!Te 2022 Kufungua Fursa Za Utalii

23 October 2022, 9:47 am

NAIBU Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) amesema uwepo Onesho la Kimataifa la Utalii la Swahili (S!TE) katika Jiji la Dar es Salaam ni fursa kubwa kwa jijini hilo kutangaza vivutio vyake.

Amesema kuwa Jiji la Dar es Salaam ndio lango Kuu la Biashara Tanzania na kwamba wageni wengi wanaofika nchini wanafikia katika Jiji hilo na kisha kuelekea kwenye maeneo mengine ya Utalii.

Mhe. Masanja ameyasema hayo alipozungumza na waandishi wa habari wakati wa mahojiano maalum yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Mlimani city Jijini Dar es Salaam kunakofanyika Onesho la S!TE 2022.

Aidha ameeleza kuwa Jiji la Dar es Salaam Lina historia ya kipekee kutokana na vivutio vilivyopo vya kiutamaduni ikiwemo majengo na malikale.

“Jiji la Dar es Salaam lina historia kubwa na nzuri ya kiutalii kutokana na uasilia wake. Kuna maeneo mengi ya kiutalii ikiwemo majengo na malikale hivyo Onesho hili litafungua fursa za kiutalii katika Jiji hili” amesema Mhe. Masanja.

Akizungumzia Onesho hilo Naibu Waziri huyo amesema Lengo kuu la Onesho hilo ni kutangaza vivutio vya utalii vilivyoko nchini Tanzania, na kukutanisha wanunuzi na wauzaji wa bidhaa za utalii wa Kitaifa na Kimataifa.