Nuru FM

EBOLA: Tuchukue Tahadhari Sahihi

13 October 2022, 5:43 am

Wataalamu wa Afya wametakiwa kujua ugonjwa wa Ebola na kuwaelimisha wengine ili kujua jinsi ya kujikinga pamoja na kuchukua tahadhari sahihi namna ya kukabiliana na ugonjwa huo.

Hayo ameyasema Mganga Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dkt. Urio Kusirye wakati akifungua mafunzo ya kuijengea uwezo timu ya matibabu ya magonjwa ya mlipuko na jinsi ya kujikinga na kudhibiti maambukizi ya ugonjwa ikiwemo tishio la Ebola.

“Magonjwa mengi ya mlipuko yanapotokea huwa yanaathiri huduma nyingine, tunapaswa kuchukua elimu hii na kwenda kuielimisha jamii katika Mikoa yetu tuliyotoka.” Amesema Dkt. Kusirye

Aidha, Dkt. Kusirye amesema kuwa matarajio ya Serikali ni makubwa baada ya kutolewa kwa mafunzo hayo kutoka kwa wataalamu wa Afya kwa kushirikiana na Shirika la Afya Duniani (WHO).

“Morogoro ni katikati ya Mikoa mingi na magari (maroli) yanayopita hapa sio chini ya elfu Saba kwa siku kutoka sehemu mbalimbali ndani na nje ya nchi hivyo niwaombe sana tupambane tuzuie ugonjwa huu usiingie nchini.”

Hata hivyo, Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Shirika la Afya Duniani (WHO) imelenga kutoa mafunzo hayo kwa Wataalamu wa Afya ambao ni wakufunzi ngazi ya Taifa kwa lengo la kwenda kutoa elimu hiyo katika Mikoa husika.

Wakufunzi hao waliochaguliwa ni watumishi kutoka katika Hospitali ya Taifa, Hospitali za Kanda, Hospital Maalumu na Hospitali za Rufaa za Mikoa nchi nzima ambapo kwa sasa wameanza na Mikoa 12.

Wataalamu kwa kundi la kwanza limewajumuisha wataalamu kutoka Morogoro, Dar es Salaam, Mbeya, Kilimanjaro, Iringa, Dodoma, Kagera, Mwanza, Mara, Geita, Songwe na Pwani.