Nuru FM

Taasisi ya RUFFO yaendesha kampeni ya kuchangia taulo za kike kuwarudisha wanafunzi shuleni

11 July 2022, 8:02 am

Taasisi ya Raising Up Friendship Foundation (RUFFO) imeitaka jamii kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kuwa na utamaduni wa kuwasaidia wanafunzi taulo za kike jambo ambalo litawasaidia kukabiliana na dharura wakati wa kuapata hedhi wakiwa shuleni.

Imeelezwa kuwa baadhi ya watoto wa keki wanakosa masomo kwa muda wa siku tano kila mwezi kutokana changamoto ya kushindwa kukabiliana na dharura ya kukosa taulo za kike wakati wakipata hedhi wakiwa shuleni.

Akizungumza hivi karibuni jijini Dar es Salaam wakati akigawa taulo za kike kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Kerezange, Mkurugenzi wa Taasisi ya Raising Up Friendship Foundation (RUFFO) Bi. Hilda Ngaja, amesema kuwa kupitia kampeni ya kuchangia taulo za kike wamefanikiwa kuwasaidia taulo wanafunzi ili waweze kuendelea na masomo wakati wakipata hedhi.

Bi. Ngaja amesema kuwa lengo ni kuhakikisha mtoto wa kike anapata haki ya afya na uzazi na kuwasaidia kuepukana na changamoto ya kuomba ruhusa ya kwenda nyumbani wakati wakipata hedhi.

“Tatizo la hedhi linakuja kama dharura, hivyo taulo za kike zitawasaidia wakiwa shuleni na kuepuka usumbufu wa kwenda nyumbani kipindi cha masomo” amesema Bi. Ngaja.

Ameeleza kuwa kupitia Kampeni ya kuchangia taulo za keki wadau mbalimbali wanapaswa kuungana na taasisi ya RUFFO kwa kuchangia taulo ili wanafunzi wa kike waendelee na masomo wakati wakipata hedhi wakiwa shuleni.

Amefafanua kuwa katika shule ya Sekondari ya Kerezange kuna wanafunzi wa keki wenye uhitaji zaidi ya 50 ambao hawana uwezo wa kupata taulo za keki, hivyo kila mwezi wanalazimika kupumzika shule siku nne hadi tano kutokana na kukosefu wa taulo za kike.

“Suala la hedhi kwa watoto wa keki ni muhimu na linapaswa kupewa kipaombele katika shule mbalimbali hapa nchini kwa kuwapatia taulo” amesema Bi. Ngaja.

Mwalimu wa Shule ya Sekondari ya Kerezange Bi. Veronica Julius, ameishukuru taasisi ya RUFFO kwa kuwapatia zawadi ya taulo za kike kwa ajili ya wanafunzi wenye uhitaji katika shule hiyo.

Bi. Julius amesema kuwa taulo hizo zitawasaidia kupunguza utolo kwa wanafunzi keki katika shule hiyo, kwani awali baadhi ya wanafunzi walikuwa hawana taulo kwa ajili ya dharura wakati mtoto anapopata changamoto.

”Tunamshukuru Mkurugenzi wa RUFFO pamoja na timu yake kwa kutusaidia taulo za kike, Mungu awabariki kwani mwanzoni tulikuwa tunapata tabu sana lakini kwa sasa taulo zinakwenda kutusaidia, naomba waendelee kutusaidia” amesema Bi. Julius.

Taasisi ya Raising Up Friendship Foundation (RUFFO) inaendelea na kampeni ya kuchangia taulo za keki kwa shule zenye wanafunzi wenye uhitaji katika Mkoa wa Dar es Salaam pmaoja na Pwani.