Nuru FM

Chuo Cha Ruaha Cdti Chashiriki Kwa Vitendo Ujenzi Wa Zahanati Kijiji Ikuvilo

4 June 2022, 7:23 am

 

CHUO cha maendeleo ya jamii Ruaha (CDTI) kwa kushirikiana na Serikali ya Kijiji cha Ikuvilo kata ya Luhota wameamua kujenga zahanati kwa lengo la kuwasogezea wananchi huduma ya afya kupatikana jirani.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwanza mkuu wa chuo cha Ruaha (CDTI) Godfrey Mafungu alisema kuwa wameamua kuunga mkono juhudi za serikali ya kijiji cha Ikuvilo na kuamua kushirikiana nao kuhakikisha wanapata huduma za afya.

Mafungu alisema kuwa wameshiriki katika hatua mbalimbali za awali za ujenzi wa zahanati hiyo ambayo itakuwa mkombozi kwa wananchi wa kijiji hicho.

Alisema kuwa malengo ya sasa ni kuhakikisha wanafanikisha ujenzi wa zahanati hiyo baada ya miezi sita huku akitoa rai kwa wananchi kuchangia shughuli za maendeleo ya kijiji.

Mafungu alisema kuwa maendeleo ya kijiji cha Ikuvilo yataletwa na wananchi wa kijiji hicho hivyo wananchi wanatakiwa kujitoa kuhakikisha wanachangia maendeleo ya kijiji.

Alisema kuwa kukamilika kwa ujenzi wa zahanati ya kijiji cha Ikuvilo kutachangia kuboresha huduma za afya na kupunguza vifo vya wananchi wa kijiji hicho kwa kuwa huduma ya afya walikuwa wanaipata umbali mkubwa.

Mafungu alimazia kwa kusema kuwa huduma ya afya ni muhimu kwa maendeleo ya jamii yote hiyo kupatikana kwa huduma hiyo wananchi watapiga hatua moja ya kimaendeleo.

 

Kwa upande wake mkufunzi wa chuo cha maendeleo ya jamii Ruaha Galiatano Alisema kuwa wananchi wa Kijiji cha Ikuvilo wanakabiliwa na tatizo la ukosefu wa huduma bora za afya hivyo chuo kikaamua kuanziasha ujenzi wa zahanati ya Kijiji hicho.

Alisema kuwa wanafanya kazi za awali kama somo kwa Wanafunzi wa chuo hicho ambacho Wanafunzi wake wanasoma masomo ambayo yanahusika katika kuhudumia jamii kwenye maendeleo.

Galiatano Alisema kuwa uongozi wa chuo cha maendeleo ya jamii Ruaha kipo tayari kufanya kazi na Serikali ya Kijiji yoyote ile bora mradi jambo liwe la jamii.

Alisema kuwa Wanafunzi na wadau wa chuo cha maendeleo ya jamii Ruaha waliojitokeza kwenye shughuli za kimaendeleo ya ujenzi wa zahanati ya Kijiji cha Ikuvilo walikuwa 277 na walifanya kazi ya uchimbaji wa msingi,utoaji wa mawe na ukusanyaji wa kokoto kutoka eneo moja hadi lingine ikiwa ishara ya ushirikiano na serikali ya Kijiji.

Rais wa Serikali Wanafunzi chuo cha maendeleo ya jamii Ruaha Jacob Arusha alisema kuwa lengo la kushirikiana na Serikali ya Kijiji cha Ikuvilo ilikuwa ni kusaidia kuboresha huduma ya afya kwa wananchi wa Kijiji hicho.

Alisema kuwa Wanafunzi wa chuo cha maendeleo ya jamii Ruaha wanafuraha kutoa mchango wao katika maendeleo ya kuboresha huduma ya afya kwa wananchi wa Kijiji cha Ikuvilo.

Arusha alisema kuwa wameamua kufanya hivyo kwa kuwa wakiwa chuoni wanasomea masomo ambayo watajihusisha na maendeleo ya wananchi.

Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Ikuvilo Meshack Mlawa alisema kuwa wananchi wanakumbana na changamoto ya ukosefu wa huduma ya afya ambayo imekuwa ileta madhala makubwa kwa wananchi.

Alisema kuwa wananchi wanasafiri umbali wa zaidi ya kilometa 18 jambo ambalo limekuwa linasababisha vifo kwa wananchi.

Mlawa alisema kuwa wanaushukuru uongozi wa chuo cha maendeleo ya jamii Ruaha kwa kukubali kushirikiana katika ujenzi wa zahanati hiyo ambayo itasaidia kuboresha huduma za afya.

Alikiri kuwepo kwa vifo vya mama na mtoto kipindi unapofika muda wa kwenda kujifungua kutokana na kuifuata huduma ya afya mbali na changamoto ya barabara.

Mlawa alisema kuwa Serikali ya Kijiji wamefanikiwa kufyatua jumla ya tofali 10040 ambazo zitatumika katika ujenzi wa zahanati hiyo na kutimiza ndoto ya Kijiji kuwa na huduma ya afya Kijiji hapo.

Alisema kuwa Kijiji hicho kinajumla ya wananchi 2699 ambao wote wanahitaji huduma ya afya kwa ajili ya maendeleo na Kijiji hicho kilisajiliwa mwaka 1978 na hakijawahi kupata huduma ya afya toka kisajiliwe.

Jane njavike mwananchi wa Kijiji cha Ikuvilo alisema kuwa wamekuwa wanapata changamoto kubwa kiasi ambacho inawabidi kusafi umbali wa zaidi ya kilomete 18.

Alisema kuwa wanawake wengi wamekuwa wanajifungulia njiani kutokana na kukosekana kwa huduma ya afya katika Kijiji hicho.

Njavike alisema kuwa wananchi wengi wamekuwa wanapoteza maisha njiani kutokana na kuifuata huduma ya afya mbali na kukumbana na changamoto ya usafi kutoka kijijini hapo hadi huduma ya afya ilipo.

Alisema kuwa kuanza kujengwa kwa zahanati ya Kijiji kwa ushirikiano Serikali ya Kijiji na chuo cha maendeleo ya jamii Ruaha kutasaidia kuokoa maisha ya wananchi wengi.

Njavike alisema kuwa anaupongeza uongozi wa chuo cha maendeleo ya jamii Ruaha kwa uamuzi wake wa kuanzisha ujenzi wa zahanati hiyo ambayo itakuwa mkombozi kwa wananchi wote.

 

Na Fredy Mgunda