Nuru FM

TBS Yatoa Mafunzo Ya Viwango Kwa Wadau Sekta Ya Utalii Kanda Ya Kaskazini

29 March 2022, 4:12 pm

Miongoni mwa sababu zinazozifanya bidhaa na huduma za nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania kushindwa kupenya na kuingia katika masoko ya kimataifa ni kushindwa kwa bidhaa na huduma hizo kukidhi matakwa ya viwango.

Ameyasema hayo leo Mkuu wa Wilaya ya Arusha Mhe.Said Mtanda wakati akifungua warsha kwa wadau wa kwenye sekta ya Utalii kwa kanda ya Kaskazini,iliyoandaliwa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika kuelekea maadhimisho ya siku ya Viwango Afrika.

Amesema wakati mwingine bidhaa na huduma hushindwa kuingia katika soko la kimataifa au la kikanda kutokana na utofauti katika matakwa ya kiwango cha bidhaa na huduma husika baina ya nchi na nchi.

“iwapo itakuwa na uwianishaji wa matakwa katika viwango baina ya nchi na nchi na hatimaye kuwa na viwango sawa kikanda na kimataifa kutawezesha uwanja wa biashara kimataifa kuwa sawia”. Amesema DC Mtanda.

Aidha DC Mtanda ameipongeza TBS kuendelea kutoa elimu ya viwango kwa wadau mbalimbali kuhakikisha bidhaa zinazozalishwa na kuingia nchini ziinakidhi viwango vinavyotakiwa.