Nuru FM

Tanzania, Liechtenstein Kuwekeza Katika Kilimo Hai

28 March 2022, 5:34 pm

Tanzania na Liechtenstein zimekubaliana kuweka mpango mkakati wa kuwekeza katika kilimo hai na kuongeza thamani ya mazao ya kilimo katika mikoa ya Morogogo na Dodoma.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (Mb) ameyasema hayo Jijini Dar es Salaam wakati alipokutana kwa mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Liechtenstein Mhe. Dominique Hasler ambaye yuko nchi kwa ziara ya kikazi.

Katika mazungumzo hayo viongozi hao wamekubalia kuangazia maeneo mapya ya ushirikiano katika sekta za Utalii, Viwanda, na Elimu, hususan kumuendeleza mtoto wa kike katika masomo ya sayansi na teknolojia.

“Tumekubaliana mara baada ya ziara yake tuweze kuangazia namna gani tunaweza kudumisha na kuendeleza maeneo mapya ya ushirikiano baina yetu kwa maslahi ya Tanzania na Liechtenstein,” Amesema balozi Mulamula.

Nae Waziri wa Mambo ya Nje wa Liechtenstein Mhe. Dominique Hasler amesema Liechtenstein ina uhusiano imara na wa siku nyingi, na tumekuwa tukisaidia miradi mbalimbali ya maendeleo iliyopo hapa nchini Tanzania hivyo kuja kwetu hap ani kuja kuiona miradi hiyo na kutuwezesha kujadiliana kwa pamoja ni namna gani tunaweza kuendele kushirikiana katika miradi hiyo.  

“Katika kikao changu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania tumejadili mambo mbalimbali ya ushirikiano baina ya nchi zetu, lakini kubwa kabisa tumekubaliana kuongeza maeneo mapya ya ushirikiano,” Amesema Waziri Hasler.

Waziri Hasler akiwa nchini atatembelea miradi mbalimbali ya kilimo hai inayotekelezwa kwa ushirikiano kati ya Tanzania na Liechtenstein kupitia Sustainable Agriculture Tanzania (SAT) katika mkoa wa Morogoro na Dodoma.