Nuru FM

Profesa Ngowi afariki dunia ajalini

28 March 2022, 5:37 pm

Profesa wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Honest Ngowi amefariki dunia leo Jumatatu Machi 28, 2022 kwa ajali ya gari iliyohusisha lori na gari ndogo alilokuwa anasafiria kwenda mkoani Morogoro.

Kamanda wa Polisi mkoani Pwani, Pius Lutumo amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kueleza imetoka eneo la Mlandizi mkoani Pwani ikihusisha magari matatu.

“Ni kweli ajali imetokea leo saa 12 alfajiri ikihusisha magari matatu aina ya Noah, Land Cruiser alilokuwa anasafiria yeye na lori ambalo ndio chanzo cha ajali lilihama njia na kuiangukia Noah ubavuni kisha kuilalia gari ya Ngowi,” amesema Lutumo

Lutumo amesema hadi wanamtoa eneo la tukio alikuwa bado mzima akawaishwa Hospitali ya Rufaa ya Tumbi Mkoa wa Pwani.

Ofisa Habari wa Chuo cha Mzumbe, Rose Mdami amethibitisha kutoka kwa kifo cha Profesa Ngowi na kwamba Makamu Mkuu wa chuo hicho Profesa Lughano Kusiluka anaelekea katika Hospitali ya Tumbi Kibaha kwa ajili ya taratibu.