Mpanda FM

Mrindoko Apiga Marufuku Watoto Kupelekwa Kumbi za Sherehe Pasaka

8 April 2023, 9:43 am

KATAVI

Mkuu wa mkoa wa Katavi Mwanamvua Hoza Mrindoko amepiga marufuku Watoto kupelekwa kwenye kumbi za sherehe katika sikukuu ya pasaka.

Akizungumza na waandishi wa Habari ofisini kwake amewataka wananchi kusheherekea sikukuu ya Pasaka kwa upendo na amani na kuhakikisha wanaweka mazingira ya usalama na kuwalinda Watoto kutokwenda katika mazingira hatarishi na kuwapeleka katika maeneo ya wazi.

Aidha Mrindoko amewataka wamiliki wa kumbi za starehe kutozidisha idadi ya watu katika maeneo yao na kusema kuwa watakaokiuka hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao ikiwemo kufungiwa ofisi zao.

Katika hatua nyingine amewataka watumiaji wa vyombo vya moto kuzingatia sheria za usalama barabarani katika kipindi hiki cha sikukuu ili kuepukana na ajali.

Aidha amewaomba wakristo kuendeleza matendo mema na kuyaishi mafunzo yote waliyokua wakiyapata katika kipindi chote cha Kwaresma.