Kitulo FM

Miche elfu 20 ya Parachichi kugawiwa kwa Walengwa wa TASAF Makambako-Njombe

January 25, 2023, 2:19 pm

Mkuu wa Mkoa wa Njombe Mhe. Antony Mtaka akizungumza na wananchi wa Makambako baada ya zoezi la kugawa miti kufanyika

Ili kukabiliana na umasikini uliopo kwenye baadhi ya familia mkoani Njombe Serikali chini ya Wizara ya Kilimo imegawa miche elfu 20 kwa kaya zinazonufaika na mpango wa TASAF Katika Halmashauri ya mji wa Makambako.

Akitoa miche hiyo katika kata ya Mlowa mkuu wa Mkoa wa Njombe Antony Mtaka amesema anataka kuona Wananchi wanaondokana na kuendelea kutegemea fedha za TASAF kwa kuwekeza kwenye kilimo cha parachichi.

Mratibu wa Tasaf  Halmashauri ya mji wa Makambako Neema Chaula amesema  Halmashauri hiyo ina walengwa wa Tasaf 1825 ambao baadhi yao wanakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo Umri mkubwa unaosababisha kushindwa kutumia simu za kupokelea fedha pamoja na vidole kutosomeka kwenye mfumo.

Baadhi ya wananchi wa kata ya Mlowa mjini Makambako pamoja na walengwa wa Tasaf akiwemo Bryton Kawogo  Alesia Chungu na Batwely Ng’umbi wanakiri kuwa miche hiyo itakwenda kuwaondoa kwenye mpango wa Tasaf  wanufaika hao .

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Njombe Kissa Kasongwa amesema atakwenda kuhakikisha walengwa hao wanaisimamia miti hiyo na ikawape matokeo chanya kwa kuwa elimu iliyotolewa na mkuu wa mkoa inawapa fursa ya kwenda kulima kwa tija.

Jumla ya miche elfu 20 ya  parachichi yenye thamani ya shilingi milioni 100 kwa walengwa wa Tasaf ambapo kila mnufaika amepata miche 10.