Kitulo FM

Kamati ya Siasa yaagiza shule iitwe Makete Boys

January 24, 2023, 6:55 am

Kamati ya Siasa Wilaya ya Makete (CCM) imeiagiza Serikali kuhakikisha shule ya Sekondari Makete ibadilishwe jina na kuitwa Makete Boys.

Agizo hilo limetolewa na Kamati hiyo tarehe 23 Januari 2023 ikiwa katika ukaguzi wa shule hiyo pamoja na kupongeza Serikali kwa ujenzi wa madarasa ya Kisasa kwa ajili ya wanafunzi.

Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Wilaya Ndg. Clement Ngajilo akiwa na wajumbe wa Kamati hiyo amesema wamekubaliana kwa pamoja wajumbe wote kuridhia mapendekezo ya wananchi kuhusu jina la shule hiyo na mfumo wa usajili wanafunzi iwe ya wavulana pekee badala ya sasa kuwa mchanganyiko.

Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilala ya Makete William Makufwe amesema kwa kuwa shule haina Bweni wala bwalo, kupitia mapato ya ndani kwa mwaka wa fedha 2023/24 imepanga kutenga Milioni 100 fedha za mapato ya ndani kwa ajili ya kujengwa bweni ili wanafunzi wawatakaoanza kuripoti kidato cha tano mwaka huu wapate sehemu ya kulala

Shule hiyo mpya iliyoanza ujenzi mwaka jana kwa fedha za SEQUIP imejengwa kwa Milioni 600 na tayari imeanza kupokea wanafunzi 65 wa Kidato cha kwanza (mchanganyiko)