Kahama FM

DODOMA:Serikali yaombwa kuanzishwa vituo vya kuhifadhia Data katika jamii.

August 29, 2021, 11:04 am

Mwanzilishi na Mkurugenzi mkuu wa Tanzania Community Nertworks Alliance Jabhera Matogoro

SERIKALI imeombwa kuanzisha na kutoa leseni kwa vituo jamii vya kuhifadhi taarifa (yaani community-owned data centre) ili kuongeza idadi maudhui ya ndani (yaani local content) ambavyo vitakuwa chachu ya kuongeza   idadi ya watumiaji wa internet kama ilivyo lengo la serikali ya awamu ya sita.

Wito huo umetolewa mwishoni mwa wiki hii jijini Dodoma na Mkurugenzi Mkuu wa Tanzania Community Nertworks Alliance Ndugu Jabhera Matogoro katika mkutano wa wadau wa huduma za mawasiliano kutoa maoni ya rasimu za marekebisho ya kanuni za leseni na maudhui mtandaoni.

Matogoro amesema kuwa yapo baadhi ya maeneo nchini hayafikiwi na huduma ya mtandao wa internet hali inayopelekea kushindwa kuhifadhi data na kutumia njia hiyo ya mawasiliano kujiongezea kipato na kukuza shughuli za ujasiliamali.

Sambamba na hayo Matogoro ametoa mapendekezo mengine kwa serikli ili kuimarisha huduma hiyo ikiwa ni Pamoja na kutoa leseni maalumu watoa huduma za mtandao jamii (yaani community networks)  kama ilivyo kwa redio na televisheni za kijamii.

Nao baadhi ya wadau wa mkutano huo Sebastian Furaha na Monica Boniphace ambao ni waandishi wa Habari za mtandaoni wamepongeza mapendekezo hayo na kwamba hiyo itasaidia maaudhui yao kusomwa vijijini ambako Habari nyingi zinaandikwa ila walengwa haziwafikii kutokana na kukosekana kwa vito vya kuhifadhia data.

Wizara ya Habari,utamaduni Sanaa na michezo iliandaa mkutano wa wadau wa huduma za mawasiliano nchini kwa lengo la kutoa maoni kwenye rasimu za marekebisho ya kanuni za leseni,kanuni za maudhui mtandaoni,kanuni za miundombinu ya utangazaji Dijitali na kanuni za maudhui-redo na televisheni.