Dodoma FM

Halmashauri zatakiwa kuhakikisha watoto wanapatiwa chanjo

30 March 2023, 7:23 pm

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dkt. Grace Magembe

Amewataka wataalamu wa afya kila wanapo kwenda kufanya huduma za mkoba lazima na huduma ya utoaji chanjo iwepo .

Na Alfred Bulahya

Serikali kupitia Wizara ya Afya imewataka Waganga wakuu wa Mikoa na Halmashauri nchini kuhakikisha watoto wote chini ya miaka mitano katika maeneo yao wanapatiwa chanjo ili kuepuka magonjwa ya milipuko.

Agizo hilo limetolewa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dkt. Grace Magembe leo Mkoani Tabora alipofanya ziara katika kituo cha Afya Maili Tano na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Kitete Tabora kwa lengo la kujionea hali ya utoaji chanjo kwa watoto chini ya miaka mitano na ubora wa huduma.

Dkt. Grace amewataka wataalamu wa afya kila wanapo kwenda kufanya huduma za mkoba lazima na huduma ya utoaji chanjo iwepo ili kuongeza kasi katika utoaji chanjo kwa watoto chini ya miaka mitano.

Sauti ya Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dkt. Grace Magembe
Wadau wa Afya wakiwa katika mkutano huo .Picha na Wizara ya Afya.

Katika Hatua nyingine Dkt. Grace ametoa pongezi kwa watumishi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Kitete Tabora pamoja na watumishi wa kituo cha Afya cha Maili Tano kwa kazi nzuri wanayofanya ya kuwatumikia Watanzania katika kutoa Huduma za afya