Dodoma FM

Wananchi wametakiwa kujitokeza kuchukua miche ya miti

9 February 2022, 3:22 pm

Na ;Thadei Tesha.

Ofisi ya maliasili jijini Dodoma kwa kushirikiana na wakala wa misitu TFS wametoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kuchukua miche ya miti kwa ajili ya kupanda kipindi hiki cha mvua.

Akizungumza na taswira ya habari afisa maliasili wa jiji la dodoma Bw Vedasto mlinga amesema ofisi yake kwa kushirikiana na wakala wa misitu tanzania TFS wameanzisha zoezi la upandaji miti ambapo kila mwananchi anao wajibu wa kutumia kipindi hiki cha mvua kupanda miti kwani miti hiyo inatolewa bure na ofisi hiyo.

Aidha amewataka wale wote wanaovuna misitu kwa ajili ya matumizi ya mkaa kufuata utaratibu wa uvunaji wa misitu ili kuendelea kutunza vyanzo vya misitu jijini hapa huku akisisitiza hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa wale wote watakaovuna misitu kinyume na utaratibu.

Kwa upande wao baaddhi ya wananchi jijini hapa wamesema ni vyema kila mwananchi kutumia fursa ya mvua katika kupanda miti ambapo wengi wao wamesema wataendelea kuwa mstari wa mbele katika kufanikisha zoezi hilo.

Miti imekuwa na umuhimu mkubwa katika maisha ya viumbe hai pamoja na kusaidia katika shughului mbalimbali za kibinadamu ambapo viongozi wamekuwa wakishirikiana na jamii kusisitiza suala la upandaji miti pamoja na utunzaji wa mazingira.